The House of Favourite Newspapers

CHIDINMA ALIZALIWA KIPOFU, LEO NI MWANAMUZIKI TAJIRI!

SAFARI ya mafanikio ina mabonde na milima, lakini ikiwa na siri kubwa ambayo ni kushikilia na kuamini kile ambacho unafikiri kitakufanya uwe miongoni mwa washindi wachache duniani, yaani waliofanikiwa.

 

Takwimu inaonesha kwamba watu waliofanikiwa duniani ni asilimia kumi ya watu wote duniani. Na ukweli ni kwamba kusikia mtu amefanikiwa inafurahisha. Mtu yeyote ukisikia juu ya mtu aliyefanikiwa unatamani kufanikiwa pia.

 

Huwa hata wengi wetu hatujiulizi kabla ya mtu huyo kufanikiwa amepitia nini mpaka kufikia mafanikio hayo. Kwa mfano pale mwanariadha wa kimataifa kutoka Jamaica, Usain Bolt anapokuwa anavunja rekodi za dunia kwa kukimbia wengi tunafurahia rekodi hizo, lakini hakuna anayeangalia saa nyingi ambazo Bolt anakuwa anatumia kufanya mazoezi kwa nguvu.

 

Haya sikia; kama ilivyo kwa watu wengi waliofanikiwa kuwa na simulizi ya kuvutia nyuma yao ambayo inakuwa ni hamasa kwa watu wengine wanaotafuta mafanikio kwa hali na mali, ndivyo ilivyo kwa mrembo na mwanamuziki kutoka Nigeria Chidinma Ekile ‘Chidinma.’

Chidinma aliyezaliwa Mei 2, 1991 ni mshindi wa Shindano la Project Fame mwaka 2010 na staa wa hit mbalimbali zikiwemo ngoma za Kalike, Fallen in Love na hapa Tanzania amewahi kufanya kazi na mwanamuziki Joh Makini.

 

Mwanadada huyu ambaye kwa sasa anaingia kwenye orodha ya wanamuziki wa kike wenye mkwanja mrefu Afrika, akimiliki zaidi ya dola za Kimarekani milioni tatu, ambazo ni sawa na bilioni 6 za Kibongo, amewahi kusimulia simulizi yake ya maisha aliyopitia ambayo inasikitisha sana.

Chidnma alisema alizaliwa akiwa kipofu na wazazi wake hawakuwa wakitegemea kwamba siku moja angeweza kupata mafanikio hayo aliyonayo.

 

Upofu wake ulimfanya hata watoto wenzake katika mitaa aliyokulia ya mji wa Ketu, pembezoni mwa Jiji la Lagos, kumcheka wakati mwingine alipokuwa akijumuika nao kucheza.

Lakini Chidnma anasimulia kwamba mama yake hakukata tamaa naye, aliendelea kukomaa akimpeleka sehemu mbalimbali za tiba mpaka siku moja akaweza kuona.

 

“Kwangu kuona lilikuwa ni suala la ajabu sana. Sikutegemea kabisa na ni kama Mungu alikuwa ameninyooshea mkono,” anasimulia Chidnma.

Chidnma anaendelea kusimulia kwamba baada ya kuona huo ndiyo ukawa mwanzo wa safari yake ya kufikia mafanikio.

Mbali na elimu akaanza kuimba kwaya kanisani na wala pia hakuwahi kuwaza kwamba angefanikiwa siku moja kuwa mwanamuziki wa kimataifa.

 

Maisha yakasonga mbele hivyo na mwaka 2010, akiwa na umri wa miaka 21, akaamua kujitupa kwenye kinyang’anyiro cha Project Fame na kuweza kufanikiwa kuibuka mshindi.

Baada ya kushinda baadaye Chidnma, ameweza kuimba wimbo uitwao Martha, ambayo ni spesho kwa ajili ya mama yake na watu wote wanaoishi na upofu duniani.

Makala: Boniphace Ngumije

Comments are closed.