The House of Favourite Newspapers

Dar: Mbaroni kwa Kukutwa na Gramu 300 za Heroin

MAMLAKA ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini inamshikilia Mohamed Hussein Gulam (48), mkazi wa Magomeni Mapipa jijini Dar es Salaam, kwa tuhuma za kukutwa na gramu 300 za dawa za kulevya zinazodhaniwa kuwa ni heroin.

 

Kwa mujibu wa Kamishna wa Intelijensia wa mamlaka hiyo, Fredick Kibuta amesema Gulam alikamatwa Agosti 16, 2018 majira ya saa 9 usiku nyumbani kwake akiwa na dawa hizo wakati akiziandaa kwa ajili ya kuziuza na baada ya kuzikamata walifanya vipimo vya awali na kuonyesha kuwa ni heroin hivyo kisha kuzipeleka kwa mkemia mkuu ili kufanya uchunguzi zaidi.

 

“Huyo mtuhumiwa bado tunamshikilia tunasubiri majibu kutoka kwa mkemia mkuu wa Serikali yakikamilika hatua za kisheria zitachukuliwa ikiwemo kufikishwa mahakamani,” amesema Kibuta.

Inadaiwa Gulam alianza biashara hiyo ya kuuza dawa za kulevya mwaka 1995 wakati huo akiishi nchini Italia ambapo alikuwa akiagiza dawa hizo Pakistani na kuzisambaza nchi mbalimbali duniani.

 

Mnamo Mwaka 1999 alirudi Tanzania na kuendelea na biashara hiyo na alikuwa akishirikiana na washirika wake kutoka Nigeria alikokuwa anauza kwa rejareja na jumla. Baada ya kuhojiwa inadaiwa ametaja baadhi ya nchi alikokuwa akiziuza dawa hizo kuwa ni Uturuki, Italia, Afrika Kusini, India na Kenya.

Comments are closed.