The House of Favourite Newspapers

DENTI ATENGWA KUTOA NYWELE KUSAIDIA WAGONJWA WA KANSA

Niamh Baldwin baada ya kunyoa nywele zake. 

MWANAFUNZI wa kike, Niamh Baldwin (14) wa shule ya Mounts Bay Academy huko Penzance, Cornwall, Uingereza, hivi sasa ametengwa na walimu na wanafunzi wenzake kwa vile alinyoa kipara na nywele zake kuzitoa kwa taasisi ya kusaidia watoto wenye kansa.

Shule yake imesema msichana huyo lazima akae nyumbani kwanza, au avae kitambaa kichwani hadi pale nywele zake zitakaporefuka. Taasisi aliyoisaidia Niamh hutengeneza mawigi kwa ajili ya watoto ambao wamepoteza nywele zao kutokana na ugonjwa wa kansa.

…Kabla ya kunyoa.

Mama yake Niamh aitwaye Anneka Baldwin (32) ameishambulia shule hiyo kwa msimamo wake huo na kusema kwamba ana fahari kubwa kwa kitendo alichokifanya binti yake.

Taasisi iliyopewa wigi hilo inaitwa Little PrincesTrust.  Msichana huyo alipofika shuleni hapo baada ya Krismasi akiwa na kipara, alitengwa na kuambiwa avae kitambaa hadi nywele zake zitakaporefuka.  Kufuatia kadhia hiyo, msichana huyo alirejea nyumbani. 

 

Pamoja na hayo, Niamh aliposti picha yake aliyonyoa kipara katika mtandao wa Facebook na kuandika: “Nywele zangu haziniongezei chochote nikiwa binadamu kama wengine.” 

 

Mama yake naye alimsifia akiandika katika mtandao huohuo: “Niamh hivi majuzi alinyoa nywele zake zote na kuipa taasisi ya kuwasaidia watoto.  Nafikiri hili ni jambo lenye ushupavu na kushangaza  zaidi.  Linanifanya niwe na fahari kubwa.  Nashangaa kwa nini wamenisononesha hivyo kwa kumtenga mtoto wangu. 

 

“Niamh amekuwa na sifa nzuri kwa walimu na watu wote ninaowafahamu ambao husema ni mpole na mwenye upendo.  Hili halibadiliki kutokana na nywele, kwa kweli kitendo hiki ni cha ubaguzi.” 

 

Akitetea msimamo wa shule yake,  mwalimu mkuu, Sara Davey, alisema sera yao kuhusu kushevu nywele iko wazi. 

 

“Wanafunzi wote wanaifahamu hii ndiyo sera ya shule na iwapo Niamh angeuliza kuhusu kunyoa nywele zake kwa ajili ya kutoa msaada, angeelezwa sera yetu na njia nyingine ya kutoa msaada wa aina hiyo ingetafutwa. 

 

“Familia yake ilikuwa na fursa zote za kuwasiliana na shule kuhusu kitendo hicho kabla ya Namh hajashevu nywele zake, lakini hawakufanya hivyo.  Hata hivyo, nitazungumza na mama yake ili Niamh aweze kurejea katika masomo,” alisema Davey. 

 

NA WALUSANGA NDAKI/MITANDAO/MASHIRIKA 

 

Comments are closed.