POLISI TANGA YAELEZEA KUCHOMWA MOTO BASI LA SIMBA COACH
JESHI la Polisi Mkoa wa Tanga limetoa ufafanuzi kuhusu tukio la kuchomwa moto kwa basi la Simba Coach.
Taarifa zinaeleza basi hilo limechomwa leo na wananchi wenye hasira baada ya dereva wake kumgonga dereva wa bodaboda.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe, amefafanua kwamba ni kweli amesikia taarifa za kuchomwa moto basi hilo lakini halijachomewa mkoani Tanga kama inavyoelezwa na baadhi ya watu.
Amesema baada ya kuona taarifa za kuchomwa basi hilo waliamua kufuatilia lakini wamejiridhisha kwamba hilo halikutokea kwenye mkoa wao bali nchini Kenya.
Amesema basi hilo lilikuwa linatoka Mombasa, Kenya, na taarifa walizonazo ni kwamba lilichomwa hukohuko Kenya kwani lilikuwa halijaingia kwenye mipaka ya Tanzania na hasa mkoani Tanga.
Alipoulizwa iwapo anafahamu namba za basi hilo na dereva aliyekuwa analiendesha, alijibu wanaendelea kufuatilia kwa polisi wa nchini Kenya na watatatoa taarifa kuufahamisha umma.
“Tunaendelea kukusanya taarifa na kwa kuwa limechomwa huko Kenya tunawasiliana na polisi wa huko ili tuwe na uhakika wa taarifa kamili za tukio hilo. Hatujapata namba za basi. Wananchi wasubiri tutaeleza kwa usahihi tutakapokamilisha kupata ukweli zinazohusu tukio hilo, ” amesema Bukombe.
Mapema asubuhi leo katika mitandao ya kijamii zilianza kuzagaa picha zinazonyesha basi linaungua moto, na ikaelezwa lilichomwa na wananchi wenye hasira mkoani Tanga lakini haikuonyesha ni sehemu gani hasa.
Ilidaiwa basi lilichomwa kwa vile dereva wake alimgonga dereva wa pikipiki na hivyo wananchi wakaonyesha hasira zao kwa kulichoma moto.
Chanzo: Michuzi
Comments are closed.