The House of Favourite Newspapers

DK. SHIKA: BATA LA UZEENI NI BALAA!

0
Dk Louis Shika

Dk Louis Shika ambaye katika siku za hivi karibuni amejipatia umaarufu mkubwa, juzikati amefunguka kuwa ‘bata’ la uzeeni analokula sasa hivi ni balaa kutokana na michongo ya fedha anayopata.

 

Akipiga stori na Risasi Jumamosi juzi, Dk. Shika alisema kuwa, wakati akisubiria fedha zake za Urusi, sasa hivi amekuwa akipata madili ya fedha na kuyabadili maisha yake.

 

Mmoja wa mameneja wa Dk. Shika ambaye hakupenda jina lake lichorwe gazetini, amethibitisha kwamba tangu aanze kumsimamia mzee huyo, amekuwa akipata michongo kibao kila siku.

 

TUMSIKILIZE MENEJA

“Daah kwa kweli ni michongo mingi sana ya hela. Yaani simu kila wakati inaita. Watu wanamhitaji kweli Dk. Shika, kwa siku napokea si chini ya simu hamsini mpaka sitini,” alisema meneja huyo.

 

AZICHUJA SIMU

Meneja huyo alisema, baada ya kuona simu hizo zimekuwa nyingi, wamelazimika kuwa wanazichuja kulingana na namna mtu anavyojieleza kwani wengi wao wamekuwa wakitoa michongo ya fedha ndogo.

 

“Unakuta mwingine anakuambia eti anataka kupiga naye picha akupe elfu tano, elfu kumi hizo kwa kweli tumelazimika kuziweka pembeni si kwamba ni ndogo lakini kwa kweli tukiruhusu hizo hatutaweza kuwahudumia wote.

WANAANZIA MILIONI

“Na badala yake tunapokea dili zile zinazoanzia milioni na kuendelea tena kwa kuangalia watu ambao wapo serious,” alisema.

DILI ALIZOWEKA KIBINDONI

Meneja huyo alisema si vyema kuzinadi dili zote na kiasi alicho nacho kwa sasa lakini akasema itoshe tu kusema kwa sasa dili za kuwaingizia mamilioni ya kutosha zimeingia na zinaendelea kuingia.

 

“Tunamshukuru Mungu kwa kweli. Amefungua milango yake tunaingiza dili za fedha. Kuna wengine wanataka tu ‘appearance’ ya muda mfupi na wengine wanataka mkataba wa muda mrefu.

 

“Mfano, Vodacom wao walituita tu ofisini kwao, tukawa na appearance pale na wafanyakazi wao, tukala nao chakula pamoja wakatulipa tukaondoka zetu.

 

ROMA NA STAMINA

“Kuna wasanii wengi wameshatufuata, wengine tupo nao kwenye mazungumzo lakini ambao tayari tumeshafanya nao kazi na imetoka ni Roma na Stamina katika wimbo wao wa Kiba 100,” alisema meneja huyo.

 

MATANGAZO YA JUISI

Sambamba na madili hayo, meneja huyo pia alisema kuna dili za bidhaa mbalimbali za juisi ambazo tayari zimeshawalipa na wameshatangaza bidhaa zao.

 

WAREMBO WAMGOMBEA

Kama hiyo haitoshi, meneja huyo alisema mbali na michongo hiyo ya fedha, warembo kibao wamekuwa wakimgombea kila wanapokatiza katika hoteli mbalimbali za kifahari wanazofika wakitaka kupiga naye picha.

 

“Unajua dokta kwa sasa kutokana na jina lake hawezi kulala sehemu moja. Analala hoteli mbalimbali za kifahari, anakula na kunywa. Sasa kila tunapopita, warembo wanamgombea wakitaka kupiga naye picha,” alisema.

 

SHIKA ALIIBUKIA WAPI?

Kwa mara ya kwanza, Dk. Shika aliibukia kwenye mnada wa nyumba za mfanyabiashara Said Lugumi zilizokuwa zikiuzwa baada ya mfanyabiashara huyo kushindwa kulipa kodi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

 

Kwenye mnada huo, Dk. Shika alifika bei katika nyumba tatu tofauti lakini hata hivyo alipotakiwa kulipia asilimia 25 kwa kila nyumba, alishindwa na kudai fedha zake zipo nchini Urusi hivyo apewe muda wa kufanya miamala.

 

ATUPWA SERO

Hata hivyo, kampuni ya udalali ya Yono Action Mart iliyokuwa na dhamana ya kusimamia mnada huo, ilimweka ndani kwa madai ya kutibua mnada, lakini hata hivyo baadaye alitoka kwa dhamana.

 

Mara baada ya kutoka polisi kwa dhamana, Dk. Shika alisisitiza kuwa ana fedha nyingi katika benki mbalimbali nchini Urusi na anaendelea na mchakato wa kuzihamishia katika benki za nyumbani ili aweze kununua nyumba hizo.

JINA LAPAA GHAFLA

Jina la Dk. Shika lilisambaa kama moto wa kifuu mara baada ya vipande vya video alivyokuwa akisikika akipanda bei kurushwa mitandaoni.

Kwenye vipande hivyo, Dk. Shika alisikika akitamka bei mbalimbali lakini Wabongo wakashikilia zaidi kile cha “mia tisa itapendeza zaidi.”

 

Dk. Shika amedai ni msomi aliyebobobea kwenye elimu ya mimea na kwamba anamiliki kiwanda cha madawa kilichopo Urusi.

Wakati huohuo, nyumba ya Lugumi ya JKT Mbweni jijini Dar es Salaam imeshindikana kuuzika kwa mara ya pili kutokana na waliotaka kuinunua kukomea Sh. Milioni 510, hivyo kushindwa kufikia kiwango kinachotakiwa na Mamlaka ya Kodi nchini (TRA).

Nyumba hiyo ilishindikana kuuzika katika mnada uliopita baada ya aliyependekeza kuinunua, Dk. Louis Shika ‘Mzee wa 900 Itapendeza’ kushindwa kutoa fedha ya awali ambayo ni asilimia 25 ya bei hivyo kuishia mikononi mwa polisi.

Mnada huo umeahirishwa tena hadi tarehe itakayotajwa

Leave A Reply