The House of Favourite Newspapers

Fahamu Kuhusu Tai Nyekundu, Blue, Zambarau Rais JPM Akiapishwa, Kufungua Bunge

0

UWANJA wa Diplomasia tumepokea maswali mengi kuhusu tai alizovaa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Magufuli wakati wa kuapishwa kwake Novemba 5, 2020 na siku ya kulifungua Bunge la 12- Novemba 13, 2020. Nasi kama jukwaa la elimu tunaona ni vema kuwasaidia wadau wetu ili kuwaongezea uelewa wa masuala ya kidiplomasia.

 

KWA NINI RAIS MAGUFULI ALIVAA TAI NYEKUNDU WAKATI ANAKULA KIAPO?

Tai nyekundu aliyovaa Rais Magufuli siku ile anakula kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Profesa Ibrahim Hamis Juma inamaanisha kuwa, alikuwa akipokea mamlaka na madaraka ama nguvu ya kuongoza nchi kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Ibara ya 8 ibara ndogo ya kwanza kifungu ‘a’ cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ambayo inasomeka kama ifuatavyo:

8.-(1) Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii, na kwa hiyo

– (a) wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, na Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii; Kimsingi tai nyekundu inamaanisha nguvu za kuongoza nchi au kutawala (power) au mamlaka au madaraka (authority).

 

KWA NINI BAADA YA KUAPA RAIS ALIBADILI TAI NA KUVAA TAI YA BLUU?

Tai ya bluu inamaanisha utulivu (serenity), uimara (stability), kuaminika/imani (reliability/trust) mwenye kuwajibika (responsible) na hekima (wisdom).

Kiongozi anapovaa tai bluu anamaanisha ana uwezo wa kusimamia nchi katika hali yoyote ile au amesimamia nchi vema na ameiacha au ameiweka katika mikono salama. Mfano Rais wa 44 wa Marekani, Barrack Obama wa Marekani alivaa tai ya bluu wakati akikabidhi nchi kwa Rais wa 45 Donald Trump ambaye alivaa tai nyekundu tarehe 20 Januari, 2017.

 

Rais Obama alimaanisha ameisimamia vema nchi na kuiacha salama huku Rais Trump alimaanisha anapokea madaraka kutoka kwa Rais Obama. Hivyo basi, Rais Magufuli alikuwa anatoa ujumbe wa kidiplomasia kwamba yeye ni kiongozi imara aliyeweza kuisimamia nchi vema Tanzania na ataendelea kuisamia vema nchi hii huku akihakikisha amani na usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hazitetereki kwa sababu ni mtulivu katika kufanya maamuzi, yupo imara, ni mtu mwenye kuaminika katika maamuzi, ni muwajibikaji na ana busara na hekima katika kufanya maamuzi yake.

TAI YA RANGI YA ZAMBARAU WAKATI WA KUFUNGUA BUNGE LA 12

Kidiplomasia rangi ya zambarau (purple) inamaanisha utajiri, milki, kitu kilichotukuka sambamba na kujiamini. Hivyo kidiplomasia Rais alikuwa anatoa ujumbe kwa mataifa mengine kuwa kupitia utajiri wa rasilimali ambazo Tanzania imebarikiwa kumiliki. Nchi hii itaweza kufikia malengo yake ya kijamii na kiuchumi.

 

Ndiyo sababu Rais aligawa hotuba aliyotoa wakati anafungua Bunge la 11 tarehe 5 Novemba, 2015 ili kuwakumbusha wabunge juu ya utekelezaji wa kazi za kibunge usimamizi wa rasilimali na pia hotuba yake ya kufungua ikiwa imeelezea mafanikio mengi ambayo Tanzania imeyafikia katika awamu hii ya tano toka alipoingia madarakani mwezi Oktoba, 2015.

 

Lakini pia tafsiri nyingine ni kuwa Tanzania ni nchi inayojiamini kwa kuwa ni dola huru (Sovereign State) ambayo haipo tayari kuyumbishwa na ambayo inatumia rasilimali zake kwa ajili ya kuwanufaisha watanzania wote. Hapa kwenye kujiamini pia kwa mujibu wa rangi ya zambarau inamaanisha kuwa Rais Magufuli anaamini ama anajiamini vizuri kuwa ametekeleza vema ilani ya uchaguzi ya chama chake bila shaka kama ilivyoelekeza.

 

Ndiyo sababu alikuwa akitoa takwimu na mambo ambayo serikali aliyoiongoza imefanya kwa wakati wote mpaka sasa. Mwisho ameipata thamani nchi yetu ya Tanzania kwa maana kidiplomasia rangi ya zambarau inamaanisha kitu kilichotukuka au cha hadhi ya juu sana (Royalty). Naamini kiu yenu imekatika ndugu zangu. Mwandishi wa makala haya ni Mhadhiri wa Chuo cha Diplomasia Dar es Salaam. Anapatikana kwa simu namba +255 719 258 484.

 

MAKALA; ABBAS MWALIMU, UWAZI

Leave A Reply