The House of Favourite Newspapers

Ibrahim Ajibu amponza Ndemla

Ibrahim Ajibu

YANGA rasmi imesitisha mpango wake wa kumsajili kiungo mkabaji, Said Ndemla katika usajili wa msimu ujao huku kiungo mshambuliaji, Ibrahim Ajibu akitajwa kuwa ndiyo sababu.

 

Timu hiyo, hivi karibuni ilielezwa kuwa kwenye mazungumzo na Ndemla ambaye hana nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza Mbelgiji, Patrick Aussems.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Spoti Xtra, viongozi wa Yanga hawataki tena wachezaji kutoka kwa watani wao Simba ni baada ya kuchukizwa na kitendo cha Ajibu kusaini Simba akiwa yupo mkataba wa kukipiga Jangwani.

 

Mtoa taarifa huyo alisema, viongozi hao akiwemo Kocha Mkuu wa timu hiyo Mkongomani, Mwinyi Zahera wamezipata taarifa hizo za kiungo huyo kusaini Simba, licha ya kufanya siri.

Aliongeza kuwa, kutokana na kitendo hicho kilichofanywa na kiungo huyo, kwa pamoja viongozi wamekubaliana na kupitisha kutomsajili Ndemla aliyekuwa kwenye mipango yao.

 

“Tunafahamu kila kitu kinachoendelea, sisi kama viongozi kwa pamoja tumekubaliana kutomsajili mchezaji yeyote kutoka Simba na hiyo ni baada ya kupata taarifa za Ajibu kusaini huko. “Hata kama ni tetesi siyo kweli, lakini Ajibu ametufundisha vitu vingi,”alisema mtoa taarifa huyo.

 

Alipotafutwa Mwenyekiti wa mpito wa timu hiyo, Lucas Mashauri kuzugumzia hilo alisema kuwa “Hilo suala lipo kwa kocha ambaye yeye ndiye atakayependekeza usajili wa wachezaji wake wapya atakaowahitaji.”

Comments are closed.