The House of Favourite Newspapers

Imethibitishwa! Pogba Kusepa Man U

KIUNGO wa Manchester United, Paul Pogba imethibitika rasmi kuwa anaondoka Manchester United. Wakala wake Mino Raiola juzi aliibuka na kusema wazi kuwa anashughulikia suala la Pogba kuihama Manchester United na kuchezea timu nyingine msimu ujao wa 2019/20.

 

Pogba akiwa Japan hivi karibuni alisema mwenyewe anataka changamoto mpya baada ya kuichezea Manchester United kwa miaka mitatu. Staa huyo alisajiliwa kwa kitita cha pauni milioni 89 kutoka Juventus mwaka 2016.

 

Manchester United imesisitiza haina mpango wa kumuuza staa huyo na kumjumuisha kwenye mipango yao ya kambi kwa ajili ya msimu ujao. Raiola, hata hivyo, amechafua hali ya hewa kwa kudai kuwa kila mtu anafahamu kuwa staa wake anataka kuondoka Manchester United.

 

“Kila mtu anafahamu dhamira ya Pogba ya kuondoka Manchester United, hakuna siri katika jambo hilo,’ alidai Raiola katika mahojiano na gazeti la Times. Raiola alisema kwa sasa ndio anaifanya kazi hiyo ya kusaka klabu kwa ajili ya Pogba.

 

Real Madrid kwa muda mrefu ndio imeonyesha nia ya kumtaka Pogba ingawa kuna taarifa ya kutakiwa na Juventus pia. Pogba bado hajaripoti kwenye kambi ya Manchester United baada ya kuongezewa siku za mapumziko kutokana na kukabiliwa na mechi za kimataifa baada ya ligi kumalizika.

 

Manchester United inatazamiwa kwenda kucheza mechi za kujipima nguvu Australia, Singapore na China na Pogba amejumuishwa kwenye listi ya watakaosafiri.

Comments are closed.