UBUYU huu umepasua anga hadi China! Baada ya hivi karibuni penzi la mastaa wa Bongo Fleva, Juma Mussa ‘Jux’ na Vanessa Mdee ‘V-Money’ kuvunjika, mwanamitindo ambaye kwa sasa yupo nyuma ya nondo za gereza nchini China, Jacqueline Patrick ‘Jack’ ametajwa.
KUMBE MAPENZI HAYAKWISHA?
Kwa mujibu wa mtoa ubuyu wetu wa kuaminika, chanzo cha Jux kuachana na Vanessa ilidaiwa kwamba ni mpenzi wa zamani wa Jux, Jack kusemekana kwamba, anatarajiwa kutoka lupango ndani ya mwezi huu hivyo jamaa huyo ana mpango wa kurudiana naye kwani wakati anakutwa na msala wa kukamatwa akisafirisha madawa ya kulevya kisha kufungwa huko Macau, China, penzi lao lilikuwa shatashata.
“Unajua Jack anatarajiwa kutoka gerezani ndani ya mwezi huu na ikumbukwe wakati anafungwa alikuwa bado kwenye uhusiano wa kimapenzi na Jux hivyo ndiyo maana mapenzi ya Jux na Vanessa yamekwisha.
“Kwa sasa Jux yupo nchini China na inasemekana atarudi na Jack kwani inadaiwa ameenda huko kwa ajili ya shughuli zake binafsi lakini pia anamsubiria Jack atoke lupango na wataendelea na mapenzi yao kama zamani,” kilidai chanzo hicho kwa sharti la kutochorwa gazetini.
WIKIENDA NA JUX
Baada ya kuunyaka ubuyu huo, Wikienda lilimtafuta Jux kwa njia ya Mtandao wa Kijamii wa WhatsApp akiwa China ambapo mahojiano yalikuwa kama ifuatavyo;
Wikienda: Mambo vipi Jux?
Jux: Poa, nani tafadhali?
Wikienda: Hapa ni kwenye Dawati la Ubuyu la Ijumaa Wikienda. Kuna habari kuwa sababu ya wewe kuachana na Vanessa ni Jack Patrick kwa sababu anatoka gerezani hivi karibuni na mapenzi yenu yataendelea kama zamani, vipi kuhusu ubuyu huo?
Jux: No coment (sina maoni).
Wikienda: Sawa, lakini pia inasemekana upo China kwa ajili ya kumpokea Jack ili urudi naye Bongo maana anatoka mwezi huu, unazungumziaje?
Jux: Sina jibu la hilo swali.
Wikienda: Kuna picha zimezagaa mitandaoni ukiwa kwenye pozi la kimahaba na wasichana wawili wa Kizungu na inasemekana mmojawapo ndiye mrithi wa Vanessa, ni kweli?
Jux: Hakuna mpenzi wangu hata mmoja. Ilikuwa ni sherehe nilipiga nao picha tu.
KUTOKA MEZA YA UBUYU
Ubuyu ndiyo huo, cha msingi ni mashabiki kusubiri kuona ukweli, lakini pia itakuwa furaha kwa wale mashabiki wa Jack ambao wana shauku ya kumuona tena kwenye video za wasanii wa Bongo Fleva na tunaamini kwa adhabu aliyotumikia gerezani atakuwa amepata fundisho la kutosha juu ya madhara ya kubeba madawa ya kulevya.
Ubuyu: Gladness Mallya | IJUMAA WIKIENDA | Dar