JB Ashiriki Igizo la Kumekucha
Na Leonard Msigwa
Msanii nguli wa filamu nchini, Jacob Steven ‘JB’ ameshiriki katika igizo la Kumekucha ambalo limeandaliwa kwa ajili ya kuhamasisha vijana kujishughulisha na kilimo kutokana na uhaba wa soko la ajira.
Katika igizo hilo, JB anatumia jina la Mzee Kidevu ambaye kazi yake kubwa ni kununua mazao kwa wakulima kwa bei ya ukandamizaji na kuwafanya wakulima hao kuendelea kuwa na maisha duni huku yeye akijinufaisha.
Akizungumza katika uzinduzi huo, JB alisema kuwa amefurahi sana kushiriki katika igizo hilo ambalo linafundisha na kuhamasisha vijana kujihusisha zaidi na masuala ya kilimo na kuacha tabia ya kukimbilia mijini kama suluhisho la kupata ajira ya kudumu.
Alisema, “Nimependa kushiriki katika igizo hili na mchezo huu wa redio, umenipa mwanga mkubwa na kupanua wigo wa kazi yangu ya kuigiza, kabla ya kuingia kwenye kuigiza, nilikuwa mnunuzi wa mazao hasa mahindi kule Kibaigwa na kusaga na kuuza unga wa chakula, hii ilikuwa fursa kwangu na nimeipenda, nawashukuru wahusika wote waliofanikisha filamu hii,” alisisitiza JB.