KAMA ilivyo kawaida ya kila wiki huwa tunakutana katika safu hii ya Mahanjumati ambapo leo tunajifunza kupika maini kama wengi wenu mlivyoomba.
MAHITAJI
Maini nusu kilo
Nyanya tano
Kitunguu kimoja
Karoti mbili
Pilipili hoho moja
Ndimu moja
Chumvi
Mafuta ya kula
KUTAYARISHA NA KUPIKA
Chukua maini yako ondoa ngozi ya juu, kata vipande kwa ukubwa unaotaka kisha yaoshe.
Kata ndimu halafu nyunyizia kwenye vipande vya maini kisha weka chumvi, hakikisha unachanganya vizuri ili yakolee.
Andaa viungo vingine (pilipili hoho, nyanya, karoti, kitunguu) vioshe na katakata vipande vidogovidogo.
Chukua sufuria safi bandika jikoni halafu weka mafuta ya kula.
Subiri mafuta yachemke kisha weka maini.
Endelea kuyakaanga huku ukiweka kitunguu, pilipili hoho na karoti.
Koroga kwa dakika tatu kisha weka nyanya.
Koroga kiasi kisha funika na mfuniko ili nyanya ziweze kuiva.
Acha kwa dakika kumi kisha epua na hapo mboga yako itakuwa tayari.
Mboga hii ni nzuri kwa kula na chapati, wali au ugali.