The House of Favourite Newspapers

KAHABA KUTOKA CHINA-08

0

Rose akaonekana kama kuchanganyikiwa, tayari hali ya hatari ikaonekana mbele yake, alijua fika kwamba baba yake alikuwa akielekea katika hostel ya Irene kwa ajili ya kumuua msichana huyo. Kwake, hakutaka kuona jambo hilo likitokea, hakutaka kumuona Irene akiuawa na baba yake, kitu ambacho alikifikiria kwa wakati huo ni kumpigia simu Irene na kumtaarifu juu ya ujio wa baba yake.

Simu angetoa wapi kwa wakati huo? Kutoka nje na kwenda kutafuta simu kwa watu wengine likaonekana kuwa jambo gumu kufanyika kwa wakati huo, angefanya nini? Kila alichokuwa akikifikiria, alikosa jibu kabisa. Rose akabaki kimya huku kichwa chake kikionekana kuwa na mawazo lukuki, alichokifikiria ambacho kilikuja kwa haraka sana kichwani kwake ni kuelekea chumbani kwa baba yake kwa ajili ya kuchukua simu yake na kisha kumpigia Irene na kumpa taarifa.

Kwa mwendo wa haraka haraka akaanza kukifuata chumba kile, alipokifikia, akakishika kitasa na kisha kujaribu kuufungua mlango, mlango ulikuwa umefungwa kwa ufunguo. Mpaka kufikia hatua hiyo Rose hakujua ni kitu gani ambacho alitakiwa kukifanya, akarudi sebuleni na kukaa kochini.

Muda bado ulikuwa ukiendelea kusogea mbele na alitakiwa kufanya jambo lile kwa haraka sana kwani kama angechelewa basi Irene angeweza kuuawa na baba yake. Rose alibaki kwa muda wa dakika kadhaa, mara akasimama kama mtu ambaye alikuwa amepata wazo jipya juu ya kitu ambacho alitakiwa kukifanya kwa wakati huo.

Kwa haraka haraka akaelekea chumbani kwake na kisha kuanza kuangalia darini. Kumbukumbu ilikuwa imejia kwamba ndani ya chumba cha baba yake, juu kulikuwa na mlango wa kuingilia darini, hivyo alitakiwa kuingia ndani ya chumba kile kwa kupitia mlango wa dari. Angeanzia wapi? Japokuwa nyumba ilikuwa yao na alikuwa ameizoea sana lakini katika kipindi hicho akaona bora kuanza kutafuta mlango mwingine wa dari.

Alipotoka chumbani kwake, kwa haraka sana akaelekea katika chumba cha John ili kuangalia kama kulikuwa na mlango wa dari, huko haukuwepo. Rose akaonekana kuchanganyikiwa kupita kawaida, muda mwingi alikuwa akiangalia saa yake ya mkononi, aliuona muda ukienda sana.

Alizunguka katika vyumba vingi vya ndani ya nyumba hiyo, hakukuwa na mlango mwingine wa dari. Huku akionekana kkata tamaa, akaonekana kukumbuka kitu, akagundua kwamba kulikuwa na chumba ambacho kilikuwa na mlango wa dari, chumba hicho kilikuwa stoo.

Bila kupoteza hata dakika moja akatoka mbio mpaka katika chumba kile, kila alipotaka kuufungua mlango ule, mlango ulikuwa umefungwa jambo ambalo lilimfanya kuanza kuzitafuta funguo katika droo za makabati yaliyokuwa pale jikoni, hakuziona funguo hizo. Akakishika tena kitasa cha mlango ule na kuanza kukitekenya, aliona kulikuwa na kila sababu ya kuuvunja mlango ule.

“Vipi tena Rose?” John ambaye alitokea mahali hapo aliuliza huku akionekana kumshangaa.

“Funguo za mlango huu zipo wapi?” Rose aliuliza huku akionekana kuchanganyikiwa.

“Wewe za nini?”

“Unaniuliza za nini tena! Niambie funguo za mlango huu zipo wapi” Rose alimwambia John huku akionekana kuchanganyikiwa.

“Zipo pale”

“Wapi?”

“Kwenye ile droo ndogo” John alimwambia Rose ambaye akaanza kuelekea katika droo ile.

Alipoifikia akaifungua na kisha kuanza kupekua pekua vizuri. Aliangalia kwa sekunde kadhaa, akauona funguo mbili, alichokifanya akzichukua na kisha kuufuata mlango ule na kuufungua. Mlango ukafunguka, alichokifanya ni kuanza kuelekea chumbani kwake na kisha kuchukua tochi na kurudi mahali pale.

“Kuna nini Rose?” John aliuliza huku akionekana kushangaa.

“Njoo unishikie hili gunia la mkaa nipande juu” Rose alimwambia John huku akimshika mkono na kumvuta.

“Unataka kwenda wapi?” john aliuliza.

“Darini”

“Darini! Kufanya nini tena?”

“Wewe njoo unishikie” Rose alimwambia John ambaye akamshikia gunia lile.

Tayari kijasho chembamba kikaanza kumtoka, kila kitu ambacho alikuwa akikifanya mahali hapo alikuwa akikifanya kwa haraka sana. Alipoukaribia mlango ule, akautoa mlango na kisha kuutoa na yeye kushika vizuri na kuingia darini.

Darini bado kulikuwa na joto kupita kawaida, Rose hakuonekana kujali kabisa, akaingia darini mule na kuanza kutembea mwendo wa kuchuchumaa chuchumaa mpaka katika usawa wa chumba cha baba yake na kuutoa mfuniko wa dari na kisha kurukia ndani.

Rose hakutaka kuchelewa, kwa haraka sana akaanza kulifuata kabati la baba yake na kisha kulifungua, akaiona simu yake na kisha kuichukua. Huku mikono ikitetemeka na huku akiwa na uharaka akaanza kulitafuta jina la ‘Hubby Irene’ alipoliona,a akabonyeza kitufe cha kijani na kisha kuipeleka simu sikioni.

Simu ikaanza kuita, Rose aliona kama Irene hapokei simu ile. Kwa uharaka ambao alikuwa nao mahali hapo, alitamani kumvuta Irene mahali alipokuwa na kisha kumgawia simu yake na kuongea nae. Alisubiria kwa zaidi na zaidi, simu ikapokelewa.

“Hallow” Sauti ya Irene ilisikika ikiita.

“Irene ondoka. Irene kimbia hapo hostel” Rose alisema huku akitetemeka kwa woga.

“Kuna nini tena? Mbona unanitisha?” Irene aliuliza.

“Baba anakuja kukuua. Kimbia, toka hapo ulipokuwa” Rose alimwambia Irene ambaye akakata simu.

Hapo, Rose akajisikia kuwa na amani, alichokifanya ni kuanza kuutafuta ufunguo mwingine wa mlango ule, alipouona, akaufungua mlango na kisha kutoka ndani ya chumba kile. Moja kwa moja akaelekea chumbani kwake huku akiwa na simu yake mkononi, alipofika akachukua nguo zake na kutoka nje.

“Umepitia wapi?” lilikuwa swali kutoka kwa John.

“Usijali” Rose alisema na kisha kuanza kupiga hatua kuelekea nje.

John akashindwa kuelewa ni kitu gani ambacho kilikuwa kikiendelea mahali hapo, alikuwa akimshangaa dada yake kwa uamuzi ule ambao aliuchukua. Mkononi alikuwa na begi na alikuwa akiondoka kuelekea sehemu ambayo yeye kama John hakuwa akiifahamu.

Rose akatoka ndani ya nyumba hiyo, begi lilikuwa mkononi mwake kwa wakati huo, alichokifanya ni kuondoka na kuelekea alipokuwa akiishi Joshua. Kitendo cha Joshua kumuona Rose akiwa amesimama mlangoni kwake huku akiwa na begi kukaonekana kumtisha, akapigwa na mshangao, hakujua sababu ambayo ilimpelekea Rose kufika mahali hapo akiwa hivyo. Alichokifanya, hakutaka kumuuliza chochote, akamkaribisha na wote kukaa kitandani.

“Kuna nini tena?” Joshua aliuliza huku akionekana kushangaa.

“Nimeondoka nyumbani mpenzi” Rose alijibu huku akianza kulia.

“Kwa nini?”

“Nimeondoka nyumbani mpenzi” Rose alimwambia Joshua.

“Najua. Kwa nini tena?”

“Sitaki kuishi pale”

“Kwa nini hutaki kuishi pale?”

“Baba ataniua”

“Mbona unanichanganya Rose. Kuna kitu gani kimetokea?”

“Naomba unielewe mpenzi. Nataka kulala hapa na kesho nitaondoka” Rose alimwambia Joshua.

“Bado unanichanganya. Unataka kuelekea wapi hasa?”

“Popote pale”

“Kama wapi?”

“Popote pale” Rose alijibu.

Katika kipindi hicho hata Joshua alionekana kuchanganyikiwa, hakujua ni kitu gani ambacho kilikuwa kimemtokea Rose mpaka kuamua kile ambacho alikuwa amekiamua mahali hapo. Rose alionekana kuchanganyikiwa, alionekana kuwa kama mtu aliyakata tamaa na ambaye alichoshwa na maisha ambayo yalikuwa yametokea nyumbani kwao.

“Naomba maji ya kunywa” Rose alimwambia Joshua.

“Hapa sina maji. Ngoja nikakununulie” Joshua alimwambia Rose na kisha kuondoka chumbani hapo, akafunga mlango kwa nje na kuondoka kwenda dukani kununua maji ya kunywa. Joshua alichukua muda wa dakika kumi, akarudi huku akiwa na maji ya lita moja na kisha kumgawia Rose ambaye akayachukua na kuanza kunywa.

Muda wote huo Joshua alikuwa akimwangalia Rose usoni, hakuonekana kuwa katika hali ya kawaida kwa wakati huo, hakuonekana kama alikuwa na furaha yoyote ile, alionekana kukata tamaa, alionekana kutokuhitaji kurudi nyumbani kwao.

Kutokana na Rose kuwa kwenye hali hiyo ambayo wala haikuonekana kuwa hali salama, Joshua akamuacha alale chumbani hapo japokuwa aliamini kwamba msichana huyo hakuwa na amani kabisa. Katika kipindi hicho hakukuonekana na mtu yeyote ambaye alionekana kuwa na uhitaji wa kufanya mapenzi japokuwa hawakuwa wameonana kwa muda mrefu sana. Wote walijikuta wakiwa wamelala chali huku wakiangalia juu.

“Kuna nini kimetokea mpenzi?” Joshua alimuuliza Rose.

“Hakuna kitu”

“Baba yako amejua kwamba una mimba?”

“Ndio” Rose alitoa jibu lilimshtua Joshua.

“Amesemaje? Hiyo ndio sababu?”

“Hapana. Alikuwa ameniandalia mtu wa kunioa”

“Hiyo ndio sababu iliyokufanya ukimbie nyumbani?”

“Hapana ila nayo imechangia” Rose alijibu.

“Pole sana mpenzi” Joshua alimwambia Rose na kisha kumkumbatia.

Walijitahidi kuuvuta usingizi lakini wala haukuonekana kupatikana kwani kila mmoja alikuwa na mawazo kwa wakati huo. Ilipofika saa sita usiku, mara wakasikia vishindo vya mtu nje ya chumba kile. Kila mmoja akaonekana kushtuka, alichokifanya Joshua ni kushuka kutoka kitandani kwa ajili ya kwenda kufungua pazia ili achungulie. Hata kabla hajalifikia pazia, sauti ya Bwana Shedrack ikasikia nje ya mlango.

“Fungua mlango. Nasema fungua mlango kabla sijauvunja” Sauti ya Bwana Shedrack ilisikika kwa nje, sauti ambayo ilikuwa na hasira kupita kawaida.

****

Bwana Joshua alikuwa akiliendesha gari lake kwa kasi sana, kichwa chake kwa wakati huo kilikuwa kimechanganyikiwa, hasira zilikuwa zimemkaba kooni hali ambayo ilimfanya mpaka kuanza kutetemeka kana kwamba alikuwa akisikia baridi. Safari hiyo ilikuwa ni kuelekea Sinza Makaburuni, mahali ambapo kulikuwa na hosteli ambayo alikuwa akiishi Irene.

Kutoka Magomeni mpaka katika hostel hiyo hakutakiwa kuchukua muda mrefu ila kutokana na kuwa na foleni za magari Tandale kwa Mtogole na Sinza Kijiweni ikamchukua dakika arobaini mpaka kufika katika sehemu ilipokuwa na jengo la hostel hiyo.

Kwa kasi ya kijeshi akateremka na kuanza kuelekea katika mlango wa kuingilia hostel hiyo huku akihakikisha kwamba bunduki yake ilikuwepo kiunoni. Alipoufikia mlango, akaanza kuugonga. Wala hazikuchukua sekunde nyingi, msichana mmoja akafika mahali hapo na kisha kuufungua mlango.

“Karibu” Msichana huyo alimkaribisha.

“Irene nimemkuta?” Lilikuwa swali lililotoka mdomoni mwa Bwana Shedrack.

“Irene yupi? Wapo Irene saba humu” Msichana yule alimuuliza Bwana Shedrack.

“Irene Godfrey”

“Mmmh! Nilimuacha bafuni anaoga kipindi fulani. Ngoja nikamwangalie” Msichana yule alimwambia Bwana Shedrack na kisha kurudi ndani. Bwana Shedrack hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuanza kumfuata msichana yule. Alijua fika kwamba endapo angefika kule na kumwambia Irene kwamba kuna mwanajeshi alikuwa amekuja kumuulizia angemfanya msichana huyo kukimbia.

Akamfuata msichana yule, akafika katika mlango wa chumba alichokuwa akiishi Irene na kisha kuugonga mlango. Mlango ulipofunguliwa, tayari Bwana Shedrack alikuwa amekwishafika, mkononi alikuwa na bunduki, akaingia ndani, akaanza kuangalia huku na kule, Irene hakuwepo.

Hakuonekana kuridhika, akatoka chumbani mule na kisha kuelekea bafuni. Kila msichana alikuwa akimshangaa, kila msichana alionekana kuogopa kupita kawaida, uwepo wa bdunduki mkononi mwa Bwana Shedrack ukaonekana kuwaogopesha. Alipofika bafuni, hakuonekana kujali, akaanza kuingia katika bafu moja mpaka jingine.

“Hayupo” Bwana Shedrack alijisemea mara baada ya kuangalia ndani ya babafu yote na vyoo, alipoona hayupo, akaondoka.

Alichokifanya ni kurudi ndani ya chumba kile. Akaishikilia vizuri bunduki yake na kisha kuanza kuwaangalia wasichana wale. Muda huo wote Bwana Shedrack alionekana kuwa na hasira, bado alikuwa akizidi kutetemeka kupita kawaida.

“Irene yupo wapi?” Ilisikika sauti ya Bwana Shedrack ikiuliza kwa hasira. Kila msichana akabaki kimya huku wote wakionekana kutetemeka kupita kawaida.

“Irene yupo wapi?” Bwana Shedrack alirudia swali lake kwa sauti ya juu iliyojaa hasira.

“Hay…up…o” msichana mmoja alijibu huku akitetemeka.

“Amekwenda wapi?”

“Alio…ndok…a..”

“Kuelekea wapi?”

“Hat..uj…u..i..”

Bwana Shedrack hakutaka kubaki, alichokifanya ni kuondoka mahali hapo. Katika kipindi hicho akaonekana kumkosa Irene ambaye alikuwa akimtafuta kupita kawaida. Akaingia garini na kisha kuondoka mahali hapo. Bado alionekana kuwa na hasira. Alipofika nyumbani, akaingia ndani.

Akaanza kuufuata mlango wa chumba chake, alipoufikia, akataka kuuingiza ufunguo, mlango ukafunguka hata kabla hajaufungua kwa ufunguo ule. Bwana Shedrack akaonekana kushtuka kupita kawaida, akaingia ndani, akawasha taa, alipoyapeleka macho yake juu, hakukuwa na mfuniko wa dari. Bwana Shedrack akaoneoakana kuchanganyikiwa zaidi, akalifungua kabati na kuangalia ndani, hata simu ya Rose haikuwepo

Kwa haraka akatoka na kisha kuelekea chumbani kwa Rose, Rose hakuwepo jambo ambalo lilionekana kumshtua kupita kwaida. Alichokifanya akaanza kueleka sebuleni, alipofika, akaanza kumwangalia John kwa macho yaliyojaa hasira.

“Rose yupo wapi?”

“Aliondoka”

“Kuelekea wapi?”

“Sijui. Aliingia darini kupitia stoo, baadae nikashtukia yupo nje na sijui alipitia wapi” John alijibu.

Bwana Shedrack akarudi chumbani, akapanda kitandani, akabaki akiwa ameegemea mto kitandani. Hakuonekana kujali kabisa kwa kitendo alichokifanya Irene cha kuondoka nyumbani pale. Ilipofika saa sita na dakika kadhaa usiku, akaonekana kuhisi kitu, akatoka chumbani na kuanza kumfuata John chumbani kwake.

“Unamjua Joshua?” Bwana Shedrack aliuliza.

“Namjua. Anaishi nyumba ya nne kutoka hapa”

“Hiyo yenye vyumba vingi?”

“Ndio” John alijibu.

Bwana Shedrack hakutaka kubaki hapo, alichokifanya ni kuondoka na kisha kuelekea chumbani kwake, akachukua bunduki yake na kisha kuondoka mahali hapo. Alipofika nje, akaanza kuelekea katika nyumba aliyokuwa akiishi Joshua, alipoifikia, akaanza kuugonga mlango wa chumba cha Joshua, alichokuwa akikitaka mahali hapo ni kuingia ndani, kumpiga sana Joshua, hata kama kumuua, haikuwa hatari, alikuwa radhi kwa hilo.

“Fungua mlango. Nasema fungua mlango kabla sijauvunja” Bwana Shedrack alisema huku akiugonga mlango kifujo fujo.

****

Irene alikuwa chumbani kwake pamoja na marafiki zake huku akiwa amevaa taulo tu. Umbo lake, makalio yake makubwa yakaonekana kutokuzoeleka katika macho ya kila msichana ambaye alikuwa akimwangalia. Alijua fika kwamba alikuwa na umbo zuri lililokuwa na mvuto, mapaja makubwa yaliyoonekana kujazia vyema hivyo alikuwa akifanya kila kitu kuwaonyeshea wasichana wenzake kwamba Mungu alikuwa ametulia sana katika kipindi ambacho alikuwa akifanya uumbaji wake.

Kila wakati alikuwa akisimama kwenye kioo kupande upande na kisha kuanza kuyaangalia makalio yake, uso wake ulikuwa ukijawa na tabasamu pana kila wakati. Mara baada ya kuona kwamba taulo lilikuwa limemkaa vizuri, akachukua maji yaliyokuwa ndani ya ndoo pamoja na kopo kisha kuanza kuelekea bafuni kuoga.

Alihakikisha kwamba kwa wakati huo anajisugua kila sehemu kwani alikuwa na mpango wa kutoka usiku huo kuelekea kwa Asha, msichana ambaye alikuwa akiishi Mwananyamala, msichana ambaye alikuwa akimchukulia kama mume wake kutokana na kumfanyia usagaji kila siku. Japokuwa Irene alikuwa kama mume kwa Rose lakini nae alikuwa na mume wake, huyu alikuwa Asha, msichana ambaye alikuwa akijulikana sana Mwananyamala kwa mchezo wake huo mchafu aliokuwa akiwafanyia wasichana wengine.

Mara baada ya kumaliza kuoga, moja kwa moja Irene akatoka bafuni mule na kueleke chumbani. Akaanza kuvaa nguo zake huku akijipulizia manukato ya bei kubwa ambayo alikuwa akiyanunua kwenye maduka makubwa yaliyokuwa jijini Dar es salaam. Huku akiendelea kujiandaa, mara simu yake ikaanza kuita.

Kwanza akapuuzia, huwa hataki kuacha kujipamba na kisha kukatisha urembo wake na kumsikiliza mtu akipiga simu. Aliendelea zaidi mpaka pale alipoona kwamba kulikuwa na umuhimu wa yeye kuipokea simu ile. Akaichukua na kisha kukiangalia kioo cha simu, jina la ‘My wifey’ lilikuwa likionekana, akatambua kwamba huyo alikuwa Rose.

Kwanza akashtuka, akabaki akijiuliza mara mbili mbili kwamba je mpigaji wa simu ile wakati ule alikuwa Rose au Bwana Shedrack? Alichokifanya ni kuipokea simu ile tena kwa tahadhari kubwa .

“Hallow” Sauti ya Irene ilisikika kinidhamu.

“Irene ondoka. Irene kimbia hapo hostel” Sauti ya Rose ilisikika simuni.

“Kuna nini tena? Mbona unanitisha?” Irene aliuliza huku akionekana kushtuka kupita kawaida.

“Baba anakuja kukuua. Kimbia, toka hapo ulipokuwa” sauti ya Rose ilisikika na simu kukatwa.

“Hallow…Hallow…!” irene aliita lakini simu haikuwa hewani.

Irene hakutaka kupuuzia hata kidogo, maneno ambayo aliambiwa na Rose yalikuwa yamemuingia sana. Akaanza kuonganisha matukio ambayo yalikuwa yametokea, tayari akajua kwamba kila kitu kilikuwa kimeharibika kwa wakati huo. Alichokifanya, akamalizia mambo yake haraka haraka na kisha kuanza kutoka nje.

“Vipi tena?” Bupe, msichana ambaye alionekana kuwa rafiki yake wa karibu alimuuliza.

“Naondoka” Irene alijibu huku akianza kukimbia.

“Wapi?”

“Baadae….” Irene alimwambia Bupe huku akizidi kukimbia kuelekea getini.

Irene akatoka nje ya uzio wa jengo lile la hostel na kisha kuanza kuangalia huku na kule, katika kipindi hicho tayari alikwishaona kwamba mambo yalikuwa yameharibika na kama angepuuzia basi Bwana Shedrack angeweza kumuua kweli. Alipoiona bajaji, akaisimamisha na kisha kuingia huku viatu vyake alivyokuwa navyo mkono akianza kuvivaa kwa haraka haraka sana.

“Wapi shemeji?” Dereva bajaji alimuuliza.

“Mwananyamala”

“Poa. Ila Mwananyamala kubwa”

“Mwananyamala A” Irene alijibu na kisha dereva kuwasha bajaji yake.

“Shilingi 4000/=”

“Wewe twende tu” Irene alimwambia na kuanza kuondoka mahali hapo.

Irene akashusha pumzi kana kwamba alikuwa amekimbia mbio ndefu, tayari aliona kufanikisha kile ambacho aliambiwa kukifanya na Rose. Katika kipindi hicho tayari hakuwa kwenye hali nzuri, alijiona kuwa mwingi wa mawazo, mwingi wa majuto kwa kila kitu ambacho alikuwa amekifanya kwa Rose. Akaanza kuyaona maisha yake yakianza kuwa ya kuangaika huku na kule kwa kuamini kwamba Bwana Shedrack asingeweza kumuacha hata mara moja, ni lazima angeendelea kumtafuta.

Walichukua dakika ishirini mpaka kufika Mwananyamala A ambapo akamlipa dereva bajaji fedha zake na kisha kuanza kuingia mitaani. Mavazi ambayo alikuwa ameyavaa katika kipindi hicho, kisketi kifupi ambacho kilikuwa kimefikia juu kabisa ya magoti yake kilikuwa kikipeperushwa na upepo kitu ambacho wakati mwingine kuyaacha mapaja yake wazi.

“Mmmh! Cheki pistol ile” kijana mmoja alisikika akimwambia rafiki yake katika kipindi ambacho Irene alikuwa akipita.

“Mbona yupo kama demu wako tu”

“Hahaha! Hapana bwana, yule kazidi utafikiri hajawahi kwenda chooni mwaka mzima”

“Hizo tamaa tu. Unaweza ukakuta yule pia ni rafiki yako facebook” Jamaa mwingine alimwambia.

Bado Irene alionekana kuwa gumzo kwa kila mvulana ambaye alikuwa akimwangalia kwa wakati huo. Mapaja yake pamoja na makalio yake yakaonekana kuwa chachu kwa kila kijana ambaye alikuwa akimwangalia. Kwa kila mtu ambaye alikuwa akipishana nae, alikuwa akigeuka na kumwangalia vizuri Irene kwa nyuma. Hata kama kulikuwa na mtu ambaye alikuwa akitembea na mpenzi wake, kila alipokuwa akipishana na Irene, kwa sababu aliona kwamba kugeuka kwa sababu mpenzi wake angemuona sio, akawa akizuga kama anafunga kabla viatu vyake ili anapoinama tu basi aweze kuyaangalia makalio ya Irene.

Mwendo wake kwa wakati huo ulikuwa ni wa haraka sana, alikuwa akitembea kwa upesi sana jambo ambalo liliyafanya makalio yake kuchezacheza sana na kuzidi kuwapagawisha wanaume ambao walikuwa wakimwangalia kwa matamanio. Hawakujua kabisa kwamba mtu ambaye walikuwa wakimwangalia alikuwa Irene, msichana ambaye alikuwa msagaji mkubwa na alikuwa rafiki wa Asha, msichana mwenye sifa za kuwasaga wasichana wengine.

“Mbona umekuja kwa kunishtukiza sana, au ulitaka kunjifumania?” Asha alimuuliza Irene mara baada ya kumtia machoni.

“Mwenzako nilitaka kuuawa” Irene alimwambia Asha.

“Na nani tena?”

“Mwanajeshi”

“Wa kiume au wa kike?”

“Wa kume”

“Umeanza lini kuchukua wanaume?”

“Sikumchukua. Nilikuwa namsaga binti yake”

“Mweeee…umekuwa kungwi kama mimi tena mke wangu?”

“Yeah! Nilikuwa najifunza”

“Sawa.Sio mbaya. Kuna jipya umekuja nalo?”

“Hapana. Ni hilo tu”

“Haiwezekani. Kuna jipya umekuja nalo mke wangu ila haujaliona” Asha alimwambia Irene huku akianza kuipeleka mikono yake kiunoni mwa Irene.

“lipi?”

“Ulivyovaa. Mavazi yako yanaeleza kila kitu” Asha alimwambia Irene na kisha kuanza kubadilishana nae mate kitendo ambacho kiliwapeleka mpaka kitandani na kisha kuanza kusagana.

Uwezo wa Asha ulikuwa ni wa juu sana, alionekana kama kusomea katika mchezo huo, akaanza kumsaga Irene ambaye muda wote alikuwa akilalamika kimahaba tu. Asha kama alikuwa na cheti cha kusagana, alikuwa amebobea mambo hayo kwa zaidi ya miaka kumi na tano kwa hiyo alikuwa na uwezo mkubwa sana. Kama kuwa na wanawake ambao aliwaita ‘wake’ basi hapo Mwananyamala alikuwa nao wengi sana ambao walikuwa wakimheshimu kama mume wao.

****

Katika kipindi ambacho Rose alikuwa akihitaji maji, Joshua akatoka na kisha kuanza kuelekea dukani. Kichwani mwake alikuwa akifikiria mambo mengi sana ambayo yalikuwa yakimsumbua kupita kawaida. Bado alikuwa akijiuliza zaidi juu ya kitendo kilichomfanya Rose kuja mahali pale kwa ghafla sana huku akionekana kwamba alikuwa amefukuzwa nyumbani. Kitendo kile kilimchanganya kupita kiasi huku mbaya zaidi akiwa anamuogopa sana Bwana Shedrack ambaye hakuwa na mchezo kwa mtoto wake.

“Inakuwaje Bingwa wa mkoa” Ally, kiajana ambaye alikuwa akiishi karibu na chumba chake alimuuliza.

“Poa. Inakuwaje wewe?”

“Kama kawa. Mbona hatuonani siku hizi japokuwa tunaishi nyumba moja?” Ally alimuuliza.

“Nipo bize sana”

“Sasa unakwenda wapi?”

“Dukani kununua maji”

“Ya shilingi ngapi?”

“Mia sita”

“Sasa toka lini umenunua maji ya mia sita, hauoni kwamba utaumwa tumbo kwa sababu halijazoea?” Ally alimtania.

“Acha zako bwana…hahah! Hapa nina msala sana”

“Msala gani?”

“Rose yupo gheto kwangu”

“Rose! Huyu mtoto wa mjeda?”

“Huyo huyo. Amekuja muda si mrefu”

“Duh! Wewe jamaa kweli noma. Sivuti picha utakavyofaidi na ule weupe pamoja na hiki kibaridi. Leo nitategesha masikio yote chumbani kwako” Ally ambaye alionekana kujaa utani alizidi kutania.

“Sikiliza. Rose hajaja kiamani, kaja na majanga Ally”

“Majanga! Majanga gani?”

“Ametoroka kwao”

“Kisa?”

“Sikijui. Ila ametoroka na kuja kulala kwangu”

“Sasa hauoni kama huo msala?”

“Ni msala ila hauna jinsi. Wakati mwingine unatakiwa kufanya maamuzi magumu hasa kwa msichana umpendae” Joshua alimwambia Ally.

Wote wakawa wamekwishafika dukani na kisha kuanza kuongea mpaka baada ya dakika kadhaa kuanza kurudi nyumbani na kila mtu kuingia chumbani kwake. Muda wote, Ally alikuwa macho, masikio yake alikuwa ametegesha kusikia ni kitu gani ambacho kingeendelea chumbani mule. Alikuwa akijua kwamba Rose alikuwa mpenzi wa Joshua na hivyo hakutakiwa kuwa na shaka, alijua tu kwamba ni lazima baada ya muda fulani kuanza kusikia sauti ambazo zingeonekana kumfariji kutokana na kibaridi ambacho kilikuwa kikimpiga muda huo.

“Mmmh! Hawaanzi tu. Muda unakwenda halafu jamaa anaremba. Au wameanza ila kimya kimya! Ngoja nipande juu kwanza nichungulie” Ally alisema.

Hapo hapo akainuka na kisha kuanza kupanga stuli yake, kwa sababu nyumba haikuwa na silling board ikamuwia wepesi kuushikilia ukuta kwa juu na kisha kuanza kuwachungulia huku kukiwa na mwanga hafifu. Alichokiona wala hakukitegemea, wote wawili walionekana kulala huku wakiangalia juu, akaonekana kukasirika.

Siku hiyo akajua fika kwamba kusingekuwa na chochote ambacho kingetokea usiku huo, akarudi kitandani na kulala. Ilipofika saa sita usiku, Ally akashtushwa na sauti ya Bwana Shedrack ambaye alikuwa akiogonga mlango kifujo fujo, tayari akajua kwamba ule ulikuwa msala mkubwa na hivyo alitakiwa kufanya kitu kimoja, kumuokoa rafiki yake kutoka kwa mzee huyo aliyeonekana kuwa na hasira za mbogo.

Kwa haraka sana Ally akateremka kutoka kitandani, akaufuata mlango wake na kisha kuanza kuufungua. Alipoufungua akatoka nje na macho yake kugongana na macho ya Bwana Shedrack ambaye bado alionekana kuwa na hasira kali.

“Shikamoo mzee” Ally alimsalimia lakini Bwana Shedrack hakuitikia.

“Fungua mlango kabla sijauvunja” Bwana Shedrack alienndelea kusema huku akionekana kuwa na hasira.

“Mwenyewe hayupo mzee” Ally alimwambia bwana Shedrack.

“Amekwenda wapi?”

“Amekwenda kupiga rusha roho Mbezi kwa Yusufu. Hajarudi mpaka sasa hivi, labda kesho asubuhi” Ally alijibu.

“Yeye ni Dj?”

“Ndio”

“Akirudi…kama akirudi mwambie roho yake halali yangu. Umesikia” Bwana Shedrack alimwambia Ally.

“Nimesikia mzee”

“Nimesemaje?”

“Akija nimwambie roho yake halali yako”

“Sawa sawa. Ukisahau hata roho yako inaweza kuwa halali yangu” Bwana Shedrack alisema na kisha kuondoka.

Ally hakutaka kujali sana, alichokuwa amekijali kilikuwa ni kumsaidia rafiki yake ili asikutwe na matatizo yoyote yale. Akarudi kulala.

Saa kumi na moja asubuhi Joshua akatoka nje pamoja na Rose. Hawakuwa wamelala toka usiku, walikuwa wakifikiria ni kipi ambacho kilitakiwa kufanyika. Walipotoka, Joshua akaelekea katika jengo la CCM na kisha kukodisha bajaji moja ya rafiki yake ambaye alitaka imfikishe Rose Sinza Makaburini.

“Kwa hiyo unakwenda kufanya nini huko?” Joshua alimuuliza.

“Nakwenda kuonana na rafiki yangu. Nadhani sitorudi tena nyumbani” Rose alimwambia Joshua.

“Sawa. Ila kuwa makini na ujauzito wangu” Joshua alimwambia Rose.

“Usijali mpenzi” Rose alisema na kisha kuingia kwenye bajaji na kuanza kuelekea katika hostel aliyokuwa akiiishi Irene huku akiwa amegawia kiasi cha shilingi laki moja na Joshua kwa ajili ya kumsaidia kwa mahitaji yake.

Baada ya kuhakikisha kwamba bajaji aliyopanda Rose ilikuwa imeondoka, akaanza kurudi kuelekea nyumbani huku kichwa chake kikiwa katika mawazo lukuki. Bado suala la Rose lilikuwa likikisumbua sana kichwa chake, hakuonekana kuwa na amani hata mara moja. Huku akiwa amefika nyumba na huku akijifikiria kuingia ndani ya ile nyumba, akasimama na kisha kuchukua simu yake, akaanza kupiga namba fulani na kuipeleka simu sikioni.

Hata kabla simu haijapokelewa, Joshua akashtuka, mwili ukampiga ganzi kubwa, akatamani kukimbia, akabaki akitetemeka kupita kawaida huku kijasho chembamba kikianza kumtoka. Bwana Shedrack alikuwa ametokea ghafla mahali hapo na kusimama mbele yake.

 

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumatatu.

Leave A Reply