The House of Favourite Newspapers

Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Afanya Ziara ya Kikazi

0
Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mabula Misungwi Nyanda akikagua gwaride Kanda ya Ziwa.

 

Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mabula Misungwi Nyanda amefanya ziara ya kikazi katika Kanda mbalimbali zilizopo TAWA ikiwemo Kanda ya Ziwa, Kanda ya Magharibi, Kanda ya Kati na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

 

Ziara hiyo ya siku tano (5) iliyofanyika kuanzia Septemba 12, 2022 hadi Septemba 17, ililenga kukagua miradi mbalimbali ya ujenzi inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali yanayosimamiwa na TAWA.

 

Akiwa katika Kanda ya Ziwa, Kamishna Mabula alikagua miradi ya ujenzi wa barabara, lango la kuingilia wageni na camping site inayotekelezwa katika Pori la Akiba Kijereshi.

Vilevile katika Pori la Akiba Maswa alikagua ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa 200, ukarabati wa kiwanja cha ndege Buruti, ukarabati wa kiwanja cha ndege Mbono, ujenzi wa kituo cha Askari, ujenzi wa ofisi pamoja na ujenzi wa vituo viwili vya kudumu vya kukabiliana na wanyama wakali na waharibifu katika vijiji vya Malwilo (Meatu) na Lugalombogo (Itilima).

 

Kadhalika katika Kanda ya Magharibi, Kamishna Mabula alikagua ujenzi wa jengo la kutoa habari (Information Center) lililopo katika Bustani ya wanyamapori Tabora (Tabora Zoo).

 

Vilevile katika Kanda ya Kati na Nyanda za Juu Kusini Kamishna Mabula alikagua ujenzi wa vituo vya kukabiliana na wanyama wakali na waharibifu vya Mtera na Mboliboli.

 

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa miradi hiyo, Kamishna Mabula amesema ameridhishwa na utekelezaji wa miradi ilipofikia na akaelekeza wakandarasi wakamilishe ujenzi wa miradi hiyo kabla ya tarehe iliyopangwa ambayo ni 31 Septemba, 2022.

 

Miradi hiyo imejengwa kwa kupitia Fedha za Maendeleo na Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO 19 na fedha za bajeti ya kawaida.

Leave A Reply