The House of Favourite Newspapers

Kamusoko, Tambwe wapewa masharti kubaki Yanga…

 

UONGOZI wa Yanga upo katika mikakati ya kuhakikisha inapitia mishahara ya wachezaji wake ili iweze kujiendesha vizuri katika msimu ujao ambapo imetoa masharti kadhaa kwa baadhi ya nyota wake wanaolipwa mishahara mikubwa ili wapunguze na kama hawatakubaliana, itaachana nao.

 

 

Miongoni mwa wachezaji wanaolipwa mishahara mikubwa huku viwango vyao vikionekana kudorora ni Thabani Kamusoko ambaye inadaiwa anakunja Sh 6,000,000 kwa mwezi, Amissi Tambwe (6,000,000), Juma Abdul (dola 2,500 ambazo ni Sh 5,767,770) na Klaus Kindoki (Sh 4,500,000).

Kwa mujibu wa chanzo chetu, kufuatia adha iliyowakumba msimu huu, hawataki tena kuendelea kujipa mizigo ambayo kwa namna fulani inakuwa mikubwa wakati inaweza kuepukika kwa kuachana na mizigo hiyo au kukaa mezani na kuona namna ya kupunguza ili waendelee nao.

 

“Uongozi wetu umedhamiria kupitia mishahara yote ya wachezaji ambapo wale waliosajiliwa kwa thamani kubwa watalazimika kupunguza ili hata wale wenye uwezo mkubwa uwanjani lakini mishahara yao midogo na wao waongezewe ili kuonyesha thamani kwa kila mmoja, kama kuna mtu atashindwa kukubaliana na hilo basi ataonyeshwa njia ya kuondokea.

 

“Kuna ambao walisajiliwa nyakati klabu ikiwa katika uchumi mzuri na kwamba walikuwa na uwezo mzuri uwanjani lakini leo hii hawapo vizuri tena, hao wataonyeshwa njia moja kwa moja, lakini ambao wapo na wana mishahara mikubwa na uwezo wao bado unakidhi mahitaji yetu hao nao tutazungumza nao ili tukubaliane kuendana na hali ya uendeshaji,” kilisema chanzo hicho.

 

Championi Jumamosi lilimsaka Msemaji wa Yanga, Dismas Ten kuzungumzia ishu hiyo, ambapo alisema mambo yote yatapitishwa baada ya uchaguzi. “Maamuzi yote yatakuja baada ya uchaguzi tukishapata viongozi wapya,” alisema Ten

MUSA MATEJA

Comments are closed.