Kanyau azidi kusota kortini
Daudi Yakubu Adam ‘Kanyau’ (aliyevaa miwani) akiwa wakili wake, John Mallya.
Stori: Mwandishi Wetu, UWAZI
Mfanyabiashara mkubwa jijini Dar aliyepandishwa Mahakama ya Kisutu jijini Dar wiki chache zilizopita kwa mashtaka ya kujipatia mali zinazodhaniwa kuibwa au kupatikana kwa njia isiyo halali, Daudi Yakubu Adam ‘Kanyau’(46), ameendelea kusota kortini baada ya kesi yake kuhairishwa tena kwa upelelezi kutokamilika.
MASHTAKA YAKE
Kanyau anayetuhumiwa kwa makosa hayo yanayotajwa kuwa kinyume cha sheria namba 16, kifungu cha 312 (1) (b) ya mwaka 2002, kesi yake iliahirishwa kwa mara ya kwanza Februari 3, mwaka huu na kupangwa kusikilizwa wiki iliyopita yaani Februari 17, mwaka huu.
Hata hivyo, baada ya kupandishwa kizimbani mbele ya hakimu mkazi wa mahakama hiyo, Thomas Simba aliambiwa kuwa kesi yake imeahirishwa tena hadi Machi 22, mwaka huu kwa kuwa upelelezi bado haujakamilika.
Kigogo huyo ambaye alipopandishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza wiki chache zilizopita alikuwa mtata kwa kuwazuia waandishi wa gazeti hili kumfotoa, zamu hii alikuwa mtulivu huku muda wote aliokuwa eneo la mahakamani hapo alivalia mawani myeusi.
Kanyau alishikiliwa kwa siku 7 na Polisi Kitengo cha Kuzuia na Kupambana na Madawa ya Kulevya, Makao Makuu, Kurasini jijini Dar es Salaam na habari za kukamatwa kwake kuandikwa kwenye Gazeti la Uwazi la Januari 19, mwaka huu huku Gazeti la Raia Mwema likichapisha kauli ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga inayomtaja kigogo huyo kuhusishwa na biashara za madawa ya kulevya.
Hata hivyo, mara baada ya habari ya Kanyau kuandikwa, kupitia mawakili wa Kampuni ya Brocard Attorneys ya jijini Dar waliliandikia Gazeti la Uwazi barua wakidai fidia ya shilingi milioni 500 kwa madai kuwa habari hiyo ni ya uongo kwani mteja wao hakuwahi kutuhumiwa, kukamatwa na polisi wala kufikishwa mahakamani.