The House of Favourite Newspapers

Kessy Agoma Kutoka First Eleven ya Lwandamina

Wilbert Molandi | CHAMPIONI|  Dar es Salaam

BAADA ya Kocha Mkuu wa Yanga, Mzambia, George Lwandamina kumuanzisha kwenye kikosi cha kwanza, beki wa pembeni Hassan Kessy, ameibuka na kutamka hataki kutoka na badala yake atapambana ndani ya uwanja kuhakikisha anaendelea kucheza.

Beki huyo, awali hakuwa anapata nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza cha Mzambia huyo na badala yake Juma Abdul ndiye aliyekuwa akianza katika kikosi cha kwanza. Kessy, mechi yake ya kwanza kuanza kucheza katika kikosi cha timu hiyo ni dhidi ya Ruvu Shooting iliyomalizika kwa Yanga kushinda mabao 2-0 na jana alianza tena kwenye mechi ya Ligi Kuu Bara Yanga ilipopambana na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Kessy alisema nafasi hiyo ameipigania kwa muda mrefu, hivyo ni wakati muafaka kwake kupambana ili aendelee kucheza katika kikosi cha kwanza. Kessy alisema, Yanga upo ushindani mkubwa wa namba, hivyo mchezaji unapopata nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza, ni lazima upambane ili umshawishi kocha aendelee kukuamini.

Aliongeza kuwa, hajawahi kukutana na changamoto kubwa ya ushindani kama aliyokutana nayo, hivyo amejifunza mambo mengi ikiwemo kutochezea nafasi atakayoipata mchezaji pale atakapoaminiwa na kuanza kucheza katika kikosi cha kwanza.

“Ujue kila timu ina ushindani wa namba, lakini huu uliopo Yanga ni mkubwa na ugeni wangu huu ndiyo uliongeza zaidi, kama unavyojua mchezaji unapojiunga na timu mpya unakuta tayari wachezaji wamejiaminisha kwa makocha na viongozi, hivyo ni lazima upambane ili umshawishi kocha akupe nafasi ya kucheza.

“Mchezaji utamshawishi kocha kwa kujituma kwako na bidii ndani ya uwanja na pale atakapokupa nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza utatakiwa kuonyesha kiwango kikubwa zaidi ya mbadala wako unayecheza naye nafasi moja.

“Hivyo, ninashukuru mechi iliyopita niliyoanza dhidi ya Ruvu nilijtahidi kupambana kwa kutimiza majukumu yangu ya ndani ya uwanja ikiwemo kuokoa hatari na kupunguza na kuanzisha mashambulizi kwenye goli la wapinzani wetu,” alisema Kessy.

Comments are closed.