The House of Favourite Newspapers

Walichozungumza Marais Magufuli, Ndayishimiye Kigoma – Video

0

MARAIS John Pombe Magufuli wa Tanzania na Evariste Ndayishimiye wa Burundi wamesema ushirikiano baina ya mataifa hayo yanayounda Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ni wa kindugu unaopaswa kuendelezwa.

 

Viongozi hao wamesema hayo leo Jumamosi tarehe 19 Septemba 2020 katika Uwanja wa Lake Tanganyika Mkoa wa Kigoma walipokuwa wakizungumza na wananchi na Watanzania.

 

Ndayishimiye ametua nchini Tanzania kwa ziara ya kiserikali ya siku moja na kupokelewa na mwenyeji wake  Magufuli uwanjani hapo ambapo kabla ya kuzungumza nyimbo za mataifa hayo mawili zilipigwa na kukagua gwaride maalum.

 

 Magufuli ameanza kwa kusema “leo ni siku muhimu sana kwa Kigoma na Tanzania, Rais Ndayishimiye ameamua Tanzania iwe nchi ya kwanza kuitembelea baada ya kuchaguliwa.

 

“Amekuja hapa kwa shughuli ya mazungumzo ya Kiserikali na ndiyo maana baada ya kukaribishwa, tulitakiwa kuondoka kwenda kwenye mazungumzo kisha kwenda kuzungumza kufungua Mahakama Kuu ya Tanzania ya Kigoma.”

 

 

Magufuli ametumia fursa hiyo, kuzungumzia ushirikiano wa kibiashara kati ya Tanzania na Burundi akisema umeongezeka kutoka biashara zenye thamani ya Sh.11.5 bilioni mwaka 2016 hadi kufikia Sh.201 bilioni kwa sasa.

 

“Kituo chetu cha Uwekezaji kimesajili miradi 16 kutoka Burudi yenye thamani ya dola milioni 26.42 ambazo zimetoa ajira zaidi ya 544 na kuna taarifa zaidi ya kampuni kumi kutoka Tanzania nazo zimewekeza Burundi,” amesema.

 

Ameongeza kwambakatika mazungumzo yake na Ndayishimiye yatahusu masuala mbalimbali ikiwemo kuimarisha ushirikiano wa kibiashara kwa Burundi kuruhusu madini yake “yawe yanakuja kuuziwa hapa Kigoma na sisi Tanzania tumekwisha kufungua maduka ya madini, badala ya kupeleka nchi zingine wawe wanakuja Kigoma.

 

“Kujenga mtambo wa pamoja wa kuchenjua madini ya Nicol, Tanzania tunayo Kabanga na wao wanayo. Mazungumzo yamekwisha kuanza ili tuuze na kupata ajira na fedha,” amesema.

 

Magufuli amesema, wanajenga reli ya kutoka Uvinza – Msongati hadi Kitega “tunataka watu wa Kigoma wakitaka kusafiri watumie ndege, maji au barabara na tayari ndege za ATCL zimekwisha kuanza kwenda Burundi.

 

“Sisi tunataka kuitengeneza Kigoma kuwa HUB ya biashara. Tunataka kujenga uwanja mkubwa wa ndege ili ikitoka Dar es Salaam inatua Kigoma inakwenda Bujumbura.”

 

Kwa upande wake,Ndayishimiye amesema “nina furaha sana sana kuwa hapa kwa wazazi wetu Tanzania. Naomba msamaha labda Kiswahili changu kitakuwa kibovu. Mimi sikuzaliwa karibu na mpaka wa Tanzania lakini nitajitahidi.”

 

Amesema, zamani Watanzania wakiona Warundi wanakwenda Kigoma walidhani kuna matatizo “lakini leo nimekuja wanawasalimia sana.

 

“Nikupongeze kabisa kwa sababu umeijenga Tanzania, umebadilisha Tanzania. Mimi nilikuwa nakuja hapa Kigoma na familia yangu ilikuwa inakuja hapa na kwa muda mchache tu, naona Kigoma imebadilika.

 

“Nakupongeza sana na nakupa pole kwa mchoko wa kampeni, nina uhakika wananchi wa Tanzania ni kama baba na watoto na nina uhakika sana utashinda uchaguzi tena sana na Warundi wote wanasema ningekuwepo ningechagua Dk. John Pombe Magufuli,” aliseme akiibua shangwe uwanjani hapo.

 

Ameendelea kusema, “nimekuja hapa kwa sababu Tanzania siyo kusema ni rafiki tu, bali Watanzania wote ni ndugu na Burundi tunasema Watanzania ni wazazi kwa sababu, tangu zamani katika kupambania uhuru mheshimiwa Baba wa Taifa, Julius Nyerere alikuwa anakwenda bega bega na Burundi.

 

“Wakati wa machafuko ya Burundi, Tanzania ilikubali kupokea msalaba wa Burudi na kupokea Warundi wengine na kukubali kutuombea msamaha.

 

“Tunawashukuru sana na ndiyo maana tunaona Tanzania kama wazazi na mimi ukiniona hapa, nakuona kama baba yangu na ndiyo sababu nimekuja kusoma hapa kusoma kwako ili nijue tutafanya nini.

 

Amesisitiza, “Burundi tuko tayari kufanya kazi na Tanzania na mmeamua kujenga reli ya kisasa ili mtusaidie na Kigoma mnafanya chochote ili kupata msaada wa kuendesha biashara na Burundi, tunashukuru sana.”

 

Kuhusu hali ya usalama, amesema, “kwa sasa Burundi hali ya usalama ni shwari, siyo kama zamani, Warundi wote tumekaa pamoja na kuzungumza na tukagundua, Burundi hakuna kabila la kKhutu au Watusi na tumegundua, Wazungu walitugawa tu.”

Leave A Reply