KIJANA WA SAUDIA ASHINDA DOLA 5,000 TUZO YA KIMATAIFA YA KUHIFADHI QURAN
KIJANA wa miaka 18 kutoka Saudi Arabia, Ibn Rayizah Hatim Abdullah ameibuka na kitita cha dola za Marekani 5,000 kwenye fainali za 26 za tuzo ya Kimataifa ya Quran tukufu.
Kijana Rayizah ameibuka na kitita hicho baada ya kuwashinda wenzake sita waliofanikiwa kuingia fainali hizo ambao walitoka Yemen, Zanzibar, Malaysia, Mali, Marekani na Tanzania Bara.
Nafasi ya pili imechukuliwa na kijana Hamza Soukouna (25) kutoka Mali ambaye amejishindia dola za Marekani 4,000 na ya tatu imechukuliwa na Hamza El-Habashiy (18) kutoka Marekani ambaye amejishindia dola za Marekani 3,000. Mashindano hayo yaliyoandaliwa na Jumuiya ya Kuhifadhisha Quran Tanzania, mwaka huu yalishirikisha vijana 16 kutoka nchi 16 duniani.
Akizungumza na mamia ya waumini wa Kiislamu waliofurika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee leo mchana (Jumapili, Juni 3, 2018), Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka viongozi wa dini hiyo waendelee kuwakamata vema vijana waliohifadhi Quran na kuwaendeleza kitaaluma katika fani nyingine za elimu ya kimazingira.
“Leo hii nimefarijika sana kusikia kwamba tunao vijana wetu ambao si tu wamehifadhi Quran bali pia wamehitimu fani mbalimbali katika elimu ya juu. Uwepo wa vijana wa namna hii ni muhimu katika kujenga jamii bora na yenye kuzingatia uadilifu katika kutekeleza majukumu yao,” amesema.
Amesema kazi ya kuhifadhisha Quran haiishii katika kujua kuisoma pekee. “Kuhifadhisha Quran kunapaswa kuwa msingi imara katika kujenga jamii bora kupitia mafunzo sahihi ya tabia njema, utii lakini pia kujua mipaka katika maisha yetu ya kila siku. Kwa kufanya hivyo, tutawasaidia vijana hawa tunaowahifadhisha Quran kuwa raia wema, wazalendo, wanaotambua wajibu wao, majukumu yao, kwao wenyewe na kwa nchi yao pia,” amesema.
Comments are closed.