The House of Favourite Newspapers

Kilichowabakisha Ajibu, Tshishimbi Dar Hiki Hapa

Kabamba Tshishimbi.

BAADA ya kikosi cha Yanga, juzi Alhamisi kutimkia mkoani Morogoro huku Ibrahim Ajibu na Papy Kabamba Tshishimbi wakibaki jijini Dar, kocha mkuu wa kikosi hicho, Mcongo, Mwinyi Zahera amefichua sababu za wawili hao kutoungana na wenzake.

 

Juzi Alhamisi asubuhi, Yanga ilielekea Morogoro kuweka kambi ya kujiandaa na msimu ujao wa ligi kuu pamoja na mechi zao mbili za kimataifa za Kombe la Shirikisho Afrika za Kundi D dhidi ya USM Alger na Rayon Sports.

 

Zahera ameliambia Championi Jumamosi kuwa, Tshishimbi amebaki Dar kutokana na kuwa na mazungumzo yake binafsi na uongozi huku Ajibu akisumbuliwa na malaria.

 

“Wakati tunajiandaa na safari, Ajibu alianza kumtumia picha meneja wa timu akimuonyesha kwamba yupo hospitali anaumwa malaria, lakini Tshishimbi yeye amebaki kutokana na kuwa na mazungumzo binafsi na uongozi.

 

“Tunaweza kuwakosa kabisa katika kambi yetu huku kwa sababu sijui lini watakuja, lakini kukosekana kwao kunaathiri programu yangu kwani kwenye timu akikosekana mchezaji mmoja tu ambaye yupo kwenye malengo yako inakuwa shida.

 

“Kukosekana kwao ni tatizo lakini isieleweke kwamba kwenye kikosi changu wao ni mastaa, mimi hapa sina mchezaji staa, wote ni sawa, hivyo tutaendelea na mazoezi na wachezaji waliopo lakini ni lazima uongozi uliangalie hili suala,” alisema Zahera.

 

Hata hivyo Ofisa Habari wa Yanga, Dismas Ten alisema Ajibu alikuwa akishughulikia ishu za kipolisi kutokana na duka lake kuvunjwa na wezi hivyo leo Jumamosi ataungana na wenzake huko Morogoro akiwa na Tshishimbi na Ramadhan Kabwili.

Comments are closed.