The House of Favourite Newspapers

Kindoki Ampisha Kabwili, Aanza na Biashara…

Kipa wa Yanga, Mkongomani, Klaus Kindoki.

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mkongomani, Mwinyi Zahera, amesema kuwa kipa wake Ramadhani Kabwili yupo fiti hivi sasa na kesho Alhamisi anatarajiwa kuwa sehemu ya wachezaji wake atakaowaanzisha katika kikosi chake cha kwanza.

 

Yanga kesho Alhamisi inatarajiwa kujitupa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kuvaana na Biashara FC katika mchezo wa FA.

 

Kipa huyo alikuwa nje ya uwanja kwa muda wa wiki mbili akiuguza maumivu ya misuli huku akikosa baadhi ya michezo ya Ligi Kuu Bara.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Zahera alisema kipa wake huyo alianza mazoezi magumu ya timu tangu wiki iliyopita kabla ya kesho kumuanzisha katika mchezo huo.

 

Zahera alisema kuwa maandalizi ya kikosi chake yanaendelea vizuri na kikubwa katika mchezo huo anahitaji ushindi pekee ili waendelee katika hatua inayofuata ya michuano hiyo.

 

“Ni habari njema kwa mashabiki wa Yanga kuwa, kipa wao Kabwili amepona majeraha yake na yupo fiti kwa ajili ya kuipambania timu yake.

 

“Hivyo, kesho Alhamisi anatarajiwa kuwa sehemu ya kikosi chake cha kwanza kitakachoanza kucheza na Biashara kwenye Uwanja wa Taifa,” alisema Zahera.

Wilbert Molandi

Comments are closed.