The House of Favourite Newspapers

Kisa Mtoto, Joti Mzazi Mwenzake Hapatoshi

Mchekeshaji mahiri Bongo Lucas Mhuvile ‘Joti’ akiwa na mke wake wa sasa

MADAI mazito yameibuka kuwa mchekeshaji mahiri Bongo Lucas Mhuvile ‘Joti’ ambaye siku chache zilizopita alifunga pingu za maisha, juzikati palikuwa hapatoshi kati yake na mzazi mwenzake, Melisa Bushoke wakimgombea mtoto wao, Loveness.

 

Kwa mujibu wa chanzo kilicho karibu na msanii huyo kilisema kuwa mtoto wao huyo ambaye anasoma shule za bweni, kwa kawaida siku za likizo huchagua sehemu ya kukaa kati ya baba na mama yake na safari hii, alikuwa ameenda kwa mzazi wake wa kiume.

 

“Sasa unajua huyu mama wa mtoto, mama yake mzazi (bibi wa mtoto) anaishi Afrika Kusini, alikuwa anataka mjukuu wake aende akamtembelee maana ni siku nyingi hajamuona, hivyo akaja kwa mzazi mwenzake na kumuomba amruhusu mtoto aende Sauzi, hapo ndipo ikawa shida, baba mtu akakomaa hataki mtoto wake aende kokote msimu huu wa sikukuu,” kilisema chanzo hicho na kusema suala hilo lilizua mtafaruku mkubwa.

 

Joti, mmoja wa wachekeshaji wazuri na wenye mikataba mingi ya matangazo nchini kwa sasa, alitafutwa kupitia simu yake ya mkononi, lakini hakupokea na hata alipotumiwa ujumbe kwa njia ya WhatsApp, hakujibu ingawa ulionekana kuwa umesomwa.

 

Kwa upande wake, Melisa alipotafutwa, alikiri kutokea kwa tukio hilo, akidai kuwa ni kweli mama yake mzazi (bibi wa Loveness) anayeishi Afrika Kusini, alihitaji kumuona mjukuu wake, lakini mzazi mwenzake huyo hakuwa tayari kuridhia ombi hilo, hali iliyosababisha kutokuelewana kidogo.

 

“Mtoto muda mwingi yupo shule bweni, akifunga huwa anaishi kote, kwangu na kwa baba yake, hakai sehemu moja, sasa hivi yupo kwa Joti bado, sasa nilivyomwambia nataka nimchukue mtoto akamuone bibi yake, ndiyo ikaibuka hali ya kutokuwa na maelewano baina yetu. “Sababu sipendi ugomvi nikaona isiwe shida, nimuachie mwanaye, naamini ipo siku atajisikia kumleta akamuone bibi yake,”alisema Melisa na kukata simu.

Comments are closed.