The House of Favourite Newspapers

Kisa Yondani, Mbelgiji Simba Amuweka Kitimoto Okwi

Patrick Aussems

KATIKA kuelekea mpambano wa watani wa jadi Simba na Yanga, Kocha Mkuu wa Simba Mbelgiji, Patrick Aussems jana Ijumaa alimuweka kitimoto mshambuliaji wake Mganda, Emmanuel Okwi.

 

Tukio hilo la aina yake lilitokea dakika chache mara baada ya kupuliza filimbi ya kumaliza mazoezi ya timu hiyo yaliyofanyika jana asubuhi kwenye Viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam.

 

Timu hizo zinatarajiwa kuvaana kesho Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam katika mchezo wa Ligi Kuu Bara utakaoanza kupigwa saa 11 jioni. Kocha huyo baada ya mazoezi hayo kumalizika alimuita Okwi na kumtaka abaki naye uwanjani wakiwa wawili pekee yao na kikubwa alikuwa akizungumza naye huku akimpa maelekezo kwa vitendo.

Mshambuliaji Mganda, Emmanuel Okwi.

Wakiwa uwanjani hapo, kocha huyo alikuwa akimpa maelekezo ya njia ya kushambulia wakati timu yao ikiwa na mpira ikishambulia goli la wapinzani wao huku akitumia mikono yake kumuonyeshea kwa vitendo.

 

Akifuatilia maelekezo hayo, Okwi alionekana akiitikia kwa kichwa akimaanisha kuwa anamuelewa kabla ya baadaye kuelekea nje ya uwanja kwa ajili ya kufuata programu nyingine ya mazoezi ya viungo.

 

Tukio hilo la aina yake lilichukua dakika kumi kabla ya kocha huyo na Okwi kutoka nje ya uwanja na kuendelea na utaratibu mwingine na baadaye kwenda kwenye basi tayari kuondoka uwanjani hapo.

 

Okwi mara nyingi amekuwa akipata wakati mgumu anapopambana na Yondani pindi timu zao zinapocheza kwani mara nyingi kila mmoja anataka kumuonyesha mwenzake uwezo wa kumzuia.

Comments are closed.