The House of Favourite Newspapers

KITENGE WA STAND: JUUKO SIYO MTU MZURI

STRAIKA wa Stand United, raia wa Burundi, Alex Kitenge amefunguka kuwa alishindwa kuwafunga Simba kwenye mchezo wao uliopigwa wiki iliyopita Uwanja wa Taifa na timu yake kupokea kichapo cha mabao 3-0, kutokana na uimara wa safu ya ulinzi ya Simba, huku akiweka wazi kuwa Juuko Murshid ni kiboko ya mabeki wote ambao amekutana nao msimu huu.

 

Kitenge alishindwa kufurukuta tofauti na matarajio ya wengi ambapo mwanzoni mwa msimu alijiandikia historia ya kufunga mabao matatu ‘hat trick’ ya kwanza dhidi ya Yanga, licha ya timu yake kupoteza kwa mabao 4-3.

Mchezo huo uliopigwa kwenye Uwanja wa Taifa hali iliyozua mshituko kwa wapenda soka wengi na kuhisi kuwa jamaa atakuwa moto mkali katika kila mchezo.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Kitenge alisema mabeki wa Simba walimsumbua sana tofauti na alivyotarajia, huku akimtaja Mganda Juuko kuwa ni kiboko yao maana alikuwa anamfuata kila mahali ili asipate nafasi hata

 ya kutuliza mpira, kitendo ambacho alifanikiwa na mpaka mwisho wa mchezo alitoka kapa bila kuziona nyavu za Simba.

 

Kitenge aliifungukia beki ya Yanga na kudai kuwa walikuwa wanajisahau sana hali iliyosababisha yeye kupata nafasi ya kuwafunga mabao matatu, licha ya kuwa nao beki yao ipo vizuri ila walikuwa wanamsahau kitendo kilichompa nafasi ya kufunga mara kwa mara.

 

“Beki ya Simba ilinisumbua sana hasa yule Juuko alikuwa ananifuata kila mahali, alikuwa hanipi nafasi maana kila nilipokuwa naenda jamaa alikuwa nyuma yangu, alikuwa hatoki kabisa hicho ndiyo kilinipa ugumu,” alifunguka Kitenge.

Issa Liponda, Dar es Salaam.WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Comments are closed.