Kikosi cha KMC FC kesho kitashuka katika dimbani la Jamuhuri jijini Dodoma kwa ajili ya mchezo wa michuano ya kombe la Shirikisho ( ASFC) dhidi ya Dododma Jiji FC mchezo ambao utapigwa saa 16:00 jioni.
msaidizi wa Timu hiyo, Habibu Kondo amesema kuwa tayari walishafanya maandalizi ya kutosha tangu wakiwa jijini Dar es Salaam na kwamba hana hofu katika mchezo huo licha ya kwamba michuano hiyo ni migumu lakini anakiamini kikosi chake kitakwenda kufanya vizuri na hivyo kuendelea katika hatua inayofuata ya michuano hiyo ya ASFC.
Ameongeza kuwa timu anayokutana nayo kesho ni nzuri nakwamba imekuwa ikifanya vizuri katika michezo yake ya Ligi kuu hivyo pamoja na yote bado kama kocha na benchi la ufundi kwa ujumla watahakikisha kuwa Kino Boys inakwenda kufanya vizuri katika mchezo wa kesho.
“Michuano hii inafahamika kabisa kwamba ukifungwa unatoka, kwahiyo pamoja na kwamba tunakutana na timu yenye ushindani mkubwa, lakini KMC FC imejiandaa vizuri kwasababu tunahitaji kuchukua kombe hilo awamu hii, na uwezo huo tunao” amesema Habibu Kondo.
KMC inakutana kwa mara ya pili na Timu ya Dodoma Jiji ambao katika mchezo wa kwanza ulikuwa ni wa Ligi kuu soka Tanzania bara ambapo walicheza katika uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam na Kino Boys kuibuka na ushindi wa magoli mawili kwa sifuri.
Imetolewa leo Aprili 30
Na Christina Mwagala
Afisa Habari wa Timu ya KMC FC.