The House of Favourite Newspapers

Kocha Mwadui FC Apata Kigugumizi, Kisa Vichapo

0

KOCHA wa Klabu ya Mwadui, Khalid Adam amefunguka kuwa mpaka sasa bado hajajua tatizo ni nini ndani ya kikosi chake, kiasi cha kupelekea kufungwa mabao 11 ndani ya michezo miwili ya hivi karibuni huku matano kati ya hayo wakifungwa dhidi ya Simba, Jumamosi iliyopita.

 

Kabla ya kipigo cha mabao 5-0 walichokipata kutoka kwa Simba, Mwadui waliingia kwenye mchezo huo na kumbukumbu mbaya ya kupoteza mchezo wake uliopita dhidi ya JKT Tanzania kwa mabao 6-1.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu muda mfupi baada ya mchezo huo, kocha Adam alisema: “Tumefungwa jumla ya mabao 11 kwenye michezo miwili iliyopita, ni jambo la kuvunja moyo na kwa kweli binafsi sielewi ni wapi tatizo letu lilipo.

 

“Kwa sababu tulifanya marejeo mazuri ya mchezo wetu uliopita dhidi ya JKT Tanzania ambao tulipoteza kwa mabao sita, na kuelekezana nini cha kufanya ili tusirudie makosa lakini cha ajabu ni kwamba tumefanya makosa yaleyale dhidi ya Simba kiasi cha kuadhibiwa tena.

 

“Kwa sasa hakuna tunachoweza kufanya zaidi ya kukubaliana na ukweli kwamba tumepoteza mchezo wa pili mfululizo na tunatakiwa kujipanga upya kwa ajili ya michezo yetu ijayo ili kuhakikisha tunafanya vizuri.”

JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Leave A Reply