RITA FRENZEL ni mzungu raia wa Marekani ambaye anafanya kazi ya Sanaa ya vichekesho na anafanya vizuri mitandaoni kutokana na kazi yake kupendwa na kupokelewa vizuri na watazamaji.
Hivi karibuni Global TV kupitia kwa mwandishi wa habari Imelda Mtema amefanya mahojiano na Rita Frenzel anayefahamika kama Mzungu wa Mwananyamala ambapo ameongea vitu vingi ikiwemo kazi yake ya Sanaa pamoja na namna anavyoiona Tanzania.
Msani huyo ambaye ni mzaliwa wa Marekani amesema yupo nchini Tanzania kikazi ambapo kazi yake kubwa ni Sanaa ya uchekeshaji lakini mbali na hilo ni mtu ambaye anavutiwa sana na mazingira ya Tanzania ikiwemo vivutio vya utalii kama Bahari, Milima pamoja na watu wake.
Rita amesema anavutiwa sana na watanzania kwani ni wakweli na mambo yao wanayafanya kwa utaratibu mzuri tofauti na raia wa Marekani, amegusia pia kuvutiwa na chakula cha Tanzania ikiwemo Ugali, Makande, Mchicha na Wali.
Kuhusu uhusiano amebainisha kuwa hajaolewa lakini ana mpenzi wake ambaye anaishi mkoani Arusha na ndoto yake ni kuendelea kuishi nchini Tanzania kwani ameipenda sana nchi hii na hataki kurudi kwao nchini Marekani.
Kuhusu yeye kuishi Mwananyamala amesema anapenda sana kuishi maeneo hayo kwani anavutiwa sana na maeneo yenye mkusanyiko mkubwa wa watu tofauti ukilinganisha na maeneo mengine kama vile Masaki na Oyserbay.