The House of Favourite Newspapers

‘Lambalamba’ Waonywa Sumbawanga

0

WAKATI mvua zikiendelea kunyesha katika Mkoa wa Rukwa kuna baadhi ya watu, hususan wale waitwao ‘lambalamba’ wanatumia fursa hiyo kuzika vitu mbalimbali yakiwemo mapembe ya wanyama katika kona za nyumba za watu ili kuandaa mazingira ya kuja kuvifukua kipindi cha mavuno na kuwasingizia watu wanaoishi katika nyumba hizo kuwa ndiyo sababu ya kijiji kutokuwa na maendeleo.

 

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Rukwa, ACP Justin Masejo, ametoa tahadhari kwa wananchi waishio katika bonde la Ziwa Rukwa wakati Kamati ya Ulinzi na usalama Mkoa wa Rukwa ilipoambatana na Mkuu wa Mkoa huo, Joachim Wangabo, katika kukagua ujenzi na ukarabati wa barabara na madaraja katika bonde hilo.

 

Masejo alisema kuwa lambalamba huvizia nyakati za saa moja na saa mbili usiku kuzika vitu hivyo muda ambao watu wanaendelea na shughuli zao huku wengine wakiwa wametulia nyumbani mwao wakati mvua zikiendelea kunyesha na hivyo kuwataka wananchi hao kuwa makini na watu wanaofanya vitendo hivyo.

 

“Mara nyingi wanapenda kufukia kati ya saa moja usiku mpaka saa mbili wakati watu bado wanatembea ili ukimuona pembeni ya nyumba unaweza ukaona labda kapotea njia lakini kimsingi anafukia mapembe na anaweka mavitu ya rangirangi kwa maana msimu wa kiangazi ukija wanakuja kuyafukua tena na kuanza kuwaambia tena kuwa huyo mtu ni mchawi au chuma ulete, kwa hiyo wanavizia wewe umevuna mazao yako vizuri, umefuga vizuri, una duka zuri, ndipo wanaenda kufukia,” alisisitiza.

 

Aidha aliongeza kuwa zoezi hilo linafanywa kwa ushirikiano wa wanakijiji wachache wasio waaminifu na kutahadharisha kuwa asitokee mtu wa namna hiyo atakayesema kuwa anasafisha uchawi na hivyo kuwataka wanachi hao kupiga vita vituko vya namna hiyo ili kujilinda wao pamoja na mali zao.

Leave A Reply