The House of Favourite Newspapers

Mafuriko Yakata Mawasiliano Mufindi, Yakatisha Masomo kwa Wanafunzi

0
Mafuriko huko Mufindi

ZAIDI ya ekari 20 za mashamba yenye mazao mbali mbali katika kijiji cha Kitasengwa kata ya Makungu wilaya ya Mufindi mkoani Iringa, zimeharibiwa kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha mkoani humo.

 

Mwenyekiti wa kijiji hicho bwana Victor Kwihava amesema madhara mengine ya mvua hiyo yaliyotokana na maporomoko ya maji kutoka mlima Udzungwa yaliyosomba sehemu ya udongo na kufukia vivuko viwili yamesababisha kukatika kwa mawasiliano ya kitongoji cha Mwenge ziliko huduma muhimu pamoja na vitongoji vya Muongozo na cha Matumaini.

 

“Kijiji cha Mwenge ndiko ziliko huduma muhimu kwa maana ya shule ya msingi pamoja na zahanati kwa hiyo toka asubuhi kukawa hakuna mawasiliano tena na jitihada tunazoendelea nazo sasa ni kuweka sawa miundombinu”alisema Victor Kwihava

 

Mkuu wa wilaya ya Mufindi Saad Mtambule amethibitisha juu ya athari zilizotokana na mvua hizo huku akibainisha kuwa kwa sasa kumekuwa na mvua kubwa katika maeneo ya wilaya hiyo.

 

“Ni kweli na juzi,jana hadi leo kulikuwa na mvua kubwa kwenye baadhi ya maeneo lakini haswa kwenye bonde hili la Mgololo ambayo ilisababisha mito kujaa maji”amesema Mtambule.

 

Amesema miongoni mwa watu walioathirika na mvua hizo ni pamoja na watoto wa shule ambao imepelekea kukosa masomo siku ya leo.

Muonekano wa maporomoko ya maji huko Mufindi

“Tulichukua hatua kwa watoto wa shule kwasababu nimeambiwa kuna vivuko viwili vimeondolewa kwa hiyo tulizui ili wasije wakapata shida ya maji,lakini pia kuna nyumba kama ishirini ambazo ziko kwenye mkondo wa maji pia hao tumewaambia watoke waende kwenye maeneo ya milimani”alisema Mtambule.

 

Aidha amesema hakuna madhara yaliyotokea kwa binadamu zaidi ya miundombinu na mashamba huku akitoa rai kwa wananchi kuchukua tahadhari yanapotokea majanga kama hayo licha ya kujali shughuli zao.

Leave A Reply