The House of Favourite Newspapers

MAHAKIMU MBULU, WAKUMBUSHWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAO KIKAMILIFU

Jaji Mzuna akikagua majalada ya Mahakama ya mwanzo ya Endagikot wilayani Mbulu.

 

Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu- Kanda ya Arusha, Mhe. Mosses Mzuna, amewakumbusha Mahakimu kutekeleza wajibu wao ipasavyo ili kuhakikisha haki inatendeka kwa kila mwananchi na kwa wakati.

 

 

Akiwa ziarani Mahakama ya Wilaya Mbulu, Mhe. Jaji Mzuna aliwakumbusha Mahakimu wilayani humo kuwa wanapaswa kutoa adhabu kwa kuzingatia ukubwa wa kosa lenyewe na si kwa kuhamasishwa na hisia juu ya kesi husika.

 

 

“Wajibu wa kila Hakimu  ni kuhakikisha  haki inatendeka na kupitia mwenendo wa shauri na maamuzi yaliyotolewa kabla hawajaruhusu jalada kwenda kwenye ngazi nyingine za Mahakama,” alisistiza Mhe. Mzuna.

Aidha; Mhe. Jaji Mfawidhi alisisitiza juu ya umuhimu wa taarifa za mashauri kufikia wadaawa  kwa wakati unaostahili ambapo mwenendo wa shauri pamoja na nakala ya hukumu vinatakiwa viwafikie wadaawa kwa wakati.

 

Mhe. Mzuna alisema endapo taarifa hizi zitawafikia Wadaawa mapema zinawawezesha kufanya hatua nyingine kama watakuwa hawajaridhishwa na maamuzi ya Mahakama hiyo.

 

Katika kusititiza hilo Mheshimiwa Jaji Mzuna alifanya ukaguzi mdogo wa majalada ya mashauri yaliyokamilika ili kuweza kugundua ni kwa jinsi gani Mahakimu wamekuwa wakitekeleza wajibu wao.

 

 

Ukaguzi huo ulihusisha majalada ya Mahakama ya Wilaya Mbulu na majalada ya Mahakama ya mwanzo Endagikot. Pia aliwapa maelekezo na mapendekezo pale alipogundua kuna changamoto katika kutekeleza wajibu wao.

 

 

Katika ziara hiyo, Mhe. Jaji Mfawidhi alikutana pia na Wazee wa Baraza wa Wilaya ya Mbulu ili kuweza kuwafahamu na kujua changamoto wanazokabiliana nazo ambazo zinakwamisha ufanisi wa kazi zao.

 

 

Na Catherine Francis, Mahakama Kuu Arusha.

Comments are closed.