The House of Favourite Newspapers

Makambo, Mayele Kimeeleweka

0

TAARIFA zinasema kwamba, Kocha Mkuu wa Yanga, Nasredinne Nabi, ameona ili timu yake ianze kufunga mabao mengi tofauti na ilivyo sasa, ataanza kuwatumia washambuliaji wawili na si mmoja tena.

Katika uamuzi huo, washambuliaji Heritier Makambo na Fiston Mayele, ndiyo wanaotajwa kuwa chaguo la kwanza ambao Kocha Nabi atawatumia kuanzia mechi ijayo dhidi ya KMC.

Kwa siku za karibuni wakiwa mazoezini, Nabi amekuwa akiwakomalia Mayele na Makambo, ili waweze kutengeneza uwiano mzuri uwanjani na kufunga mabao mengi kwani anahitaji kuona timu ikipata ushindi mkubwa.

Chanzo chetu kutoka Kambi ya Yanga iliyopo Avic Town, Kigamboni, Dar, kimeliambia Spoti Xtra kuwa: “Kocha kwa sasa ameridhishwa na upande wa kiungo na mabeki, lakini kilio chake ni upande wa wafungaji, ambapo baada ya kumalizika kwa mechi ya kirafiki dhidi ya JKU, aliwataka wachezaji wote wanaocheza mbele kuhakikisha wanatumia vizuri nafasi za kufunga.

“Kocha hataki kabisa kwenye michezo ijayo kuona tunashinda tena bao moja moja, hivyo ameamua kuwacharukia mastraika wote na ameahidi kuanza kutumia washambuliaji wawili katika kila mechi ili aweze kutengeneza nafasi ya kuibuka na mabao mengi.”

Akizungumza na Spoti Xtra, Kocha Nabi alisema: “Tuna washambuliaji bora watatu msimu huu, kwenye kikosi yupo Makambo, Mayele na Yusuph Athuman.

“Tumeanza na matumizi ya straika mmoja kwenye michezo iliyopita, lakini tunaangalia uwezekano wa kutumia straika zaidi ya mmoja katika michezo ijayo ili kutoa nafasi zaidi kwa wachezaji wote na kuhakikisha tunatumia vema nafasi tunazotengeneza.

“Tumefanya hivyo katika mchezo wa kirafiki dhidi ya JKU, na tunaendelea kufanya tathimini ya matokeo ya maamuzi hayo ili tuanze kutumia rasmi.”

Yanga ambayo imeanza msimu vizuri kwa kushinda mechi tatu za kimashindano moja ya Ngao ya Jamii dhidi ya Simba na mbili za Ligi Kuu Bara dhidi ya Kagera Sugar na Geita Gold, lakini imekuwa ikipata ushindi kiduchu.

MUSA MATEJA NA JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Leave A Reply