Manji Amwaga Mabilioni Yanga
MWENYEKITI wa zamani wa Yanga, Yusuf Manji ni kati ya majina manne yanayotajwa kuwa tayari kuwekeza
mabilioni ya shilingi katika klabu hiyo kubwa Afrika.
Yanga hivi sasa ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha mchakato wa mfumo wa uwekezaji baada ya kuipitisha
katiba katika mkutano wao mkuu wa wanachama uliofanyika hivi karibuni.
Klabu hiyo imeishirikisha Kampuni ya La Liga ya nchini Hispania katika kufanikisha mfumo huo mpya wa mabadiliko. Mmoja wa mabosi wakubwa wenye ushawishi ndani ya Yanga, ameliambia Championi Jumatano kuwa,
wapo matajiri wakubwa wanne ambao wenyewe wapo tayari kuweka mzigo wa kutosha.
Bosi huyo aliwataja matajiri wengine ambao ni mabilionea hapa nchini ni Rostam Aziz, GSM Group Limited na Azam Group Limited.
Aliongeza kuwa mabilionea hao wote wapo katika hatua za mwisho kwa ajili ya majadiliano na uongozi huku wakisubiria mfumo kupitishwa na kuanza kufanya kazi.
“Mfumo wetu wa mabadiliko ukiwa katika hatua za mwisho za kukamilika, tayari baadhi ya mabilionea hapa nchini wenye ushawishi mkubwa wa fedha, tayari wameanza kuja kwa ajili ya uwekezaji.
“Jumla ya majina manne ya wawekezaji tayari yamefika kwa uongozi kwa ajili kuja kuwekeza Yanga katika asilimia 49 ya hisa za wawekezaji.
“Kati ya mabilionea hao yupo mwenyekiti wetu wa zamani Manji (Yusuf), Rostam, GSM
Group Limited na Azam Media Group pekee,” alisema bosi huyo.Mjumbe wa Kamati ya Mashindano ya Yanga ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM, Injinia Hersi Said hivi karibuni aliliambia gazeti hili kuwa: “Mchakato wa mabadiliko upo katika hatua za mwisho mara baada ya mkutano mkuu wa wanachama kupitisha katiba mpya, hivyo ni suala la muda pekee.”
Stori: Wilbert Molandi na Musa Mateja