The House of Favourite Newspapers

Maonyesho ya Utalii Yafunika Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kwamba maonyesho ya Utalii yanayofanyika Zanzibar ni muhimu kwa Serikali na wananchi kwa kuwa yamelenga kuitangaza Zanzibar na sekta ya utalii ambayo ndio muhimili mkuu wa uchumi.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika viwanja vya hoteli ya Verde, Mtoni Mjini Zanzibar katika ufunguzi wa maonyesho ya Utalii Zanzibar ya mwaka 2018 ambayo yalihudhuriwa na viongozi mbali mbali wakiwemo Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Makamo wa Pili wa rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, wadau wa utalii na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali pamoja na wananchi.

 

Katika maelezo hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa Utalii umekuwa ukichangia asilimia 27 kwa Pato la Taifa na asilimia 80 ya fedha za kigeni zinazokusanywa ambapo muda wanaokaa watalii nchini umeongezeka ambapo hivi sasa mtalii hutumia wastani wa siku 8 badala ya 6 kama ilivyokuwa miaka 5 iliyopita.

 

Rais Dk. Shein alieleza juhudi mbali mbali za kuimarisha utalii zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali zikiwemo kuanzisha mpango wa “Utalii kwa wote” ambapo lengo kuu la mpango huo ni kuhakikisha kwamba sekta ya utalii inawanufaisha wananchi wote wa Zanzibar na kuimarisha ustawi wa wananchi kwa jumla.

 

Alisisitiza kuwa juhudi mbali mbali zinaendelea kuchukuliwa na Serikali za kuendeleza sekta ya utalii zinaenda sambamba na mikakati na malengo ya MKUZA, Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs).

 

Alieleza imani yake kwamba maonyesho hayo ni njia bora na madhubuti ya kuitangaza Zanzibar pamoja na fursa mbali mbali zilizopo za kiuchumi kwa wawekezaji.

 

Aidha, Rais Dk. Shein aliiagiza Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale kuhakikisha kuwa watu wanaotembeza wageni wawe wamepatiwa mafunzo yanaayostahiki, wawe na vibali na wahakikiwe kila baada ya muda ili kuhakikisha kwamba hawaharibu historia ya Zanzibar kwa kuisimulia isivyo au kwa kuzingatia matakwa na utashi wao binafsi.

 

Rais Dk. Shein alieleza azma ya Serikali kulifukia eneo la babari la Gulioni kama alivyofanya mfanya biashara maarufu Said Baghresa la kufukia bahari katika eneo la Hoteli ya Verde sambamba na ujenzi wa miji ya kisasa katika eneo la Kwahani na Chumbuni na kueleza kuwa Zanzibar itabadilika sio muda mrefu.

 

Katika hafla hiyo, Rais Dk. Shein alitoa vyeti maalum kwa wadau mbali mbali waliosaidia kuutangaza utalii wa Zanzibar ndani na nje ya nchi kwa kutumia huduma wanazoziendesha yakiwemo makampuni mbali mbali, hoteli, Jumuiya na Taasisi.

 

Nae Waziri wa habari utalii na mambo ya kale Mahmoud Thabit Kombo alieleza kuwa Wizara yake imo katika hatua za kuhakikisha inavuka lengo la kufikia watalii nusu milioni kwa mwaka na kueleza kuwa lengo hilo litavukwa kwani alithibitisha kuwa hadi Julai mwaka huu walifikia watalii 263,000 ambapo wakiendelea na hatua hiyo hadi mwisho wa mwaka huu watafikia watalii 520,000.

TBC1: Alichokiona GAMBO vituo vya Kukagua Utalii

Comments are closed.