The House of Favourite Newspapers

MASTAA WALIOPITIA MISS TZ KISHA WAKAWIKA

 MASTAA wengi ambao wanawika kwenye tasnia ya filamu za Kibongo chimbuko lao ni kutoka kwenye Shindano la Miss Tanzania ambapo mpaka sasa majina yao yapo masikioni mwa watu.Baadhi ya warembo ambao walijaribu kurusha kete zao kwenye shindano hilo na kushindwa kufurukuta, leo hii majina yao yapo midomoni mwa watu mbalimbali hapa nchini kwa sababu wengi walijiingiza kwenye uigizaji;

AUNT EZEKIEL

Huyu alikuwa ni mmoja wa wawashiriki wa Miss Tanzania 2006, lakini hakuweza kufanya vizuri. Aliamua kuangalia upande mwingine wa uigizaji ambapo kwa mara ya kwanza alionekana kwenye Filamu ya Miss Bongo. Kuanzia hapo alianza kuwika na mpaka leo hii ni staa mkubwa hapa nchini.

IRENE UWOYA

Staa huyu ni miongoni mwa waliopitia kwenye Shindano la Miss Tanzania akitokea Wilaya ya Kinondoni mwaka 2006. Uwoya aliibuka kwenye tano bora, lakini baada ya hapo aliangalia upande wa filamu ambapo aliporusha karata, ikakubali na mpaka leo anawika na ana jina kubwa hapa nchini.

HAMISA MOBETO

Huyu yupo kwenye kilele cha ustaa. Alishiriki shindano hilo akitokea Wilaya ya Kinondoni. Baada ya kutoka kapa alitumbukia kwenye Bongo Movies kisha video queen na sasa anafurukuta kwenye Bongo Fleva na wimbo wake wa Madam Hero.

CHUCHU HANS

Mwigizaji huyu naye alianzia kwenye Shindano la Miss Tanzania mwaka 2005 akitokea jijini Tanga. Chuchu aliibuka kidedea kwenye Miss Talent. Baada ya hapo alijitumbukiza kwenye filamu na mpaka sasa ni mwigizaji mzuri. Alianza kutamba kwenye filamu yake ya kwanza ya Roho Sita.

LULU DIVA

Mwanadada Lulu Abbas ‘Lulu Diva’ aliingia kwenye Miss Tanzania akitokea jijini Tanga. Alipokosa taji aliamua kujiingiza kwenye muziki wa Bongo Flava na sasa ana jina kubwa kwenye muziki huo.

Wengine waliopata ‘platfom’ kupitia Miss Tanzania kisha kuingia kwenye filamu na ‘kushaini’ ni pamoja na Sylvia Shally, Miriam Jolwa ‘Jini Kabula’, Husna Idd ‘Sajent’, Husna Maulid, Isabela Mpanda, Lisa Jensen, Jack Patrick na wengine wengi. Shukurani kwa Miss Tanzania!

MAKALA: IMELDA MTEMA

Comments are closed.