The House of Favourite Newspapers

Mbaroni kwa Kuiba Laptops Saba kwa ‘Kikwete’

JESHI la polisi mkoani Pwani ,linawashilia watu watatu wanaodaiwa kuiba kompyuta mpakato saba zenye thamani ya sh. milioni 4.2 mali ya shule ya msingi Msoga iliyopo Chalinze wilayani Bagamoyo ambako ndiko kijijini kwa Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Kikwete.

 

Aidha Jeshi hilo, limewakamata watu 67 kwa tuhuma za kufanya uhalifu mbalimbali ,katika misako inayoendelea mkoani hapo.

Kamanda wa Polisi, mkoani humo Wankyo Nyigesa aliwaambia waandishi wa habari ofisini kwake, kuwa siku ya tukio watu wasiojulikana walivunja kwenye shule hiyo na kuiba vifaa hivyo.

 

Alieleza, tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki iliyopita ambapo baada ya tukio hilo uongozi wa shule ulitoa taarifa polisi ambao walianza msako na walikamata watu hao wakiwa na kompyuta tatu.

“Tunaendelea na uchunguzi kwa watu wengine ambao watakuwa na hizo kompyuta nne zilizobakia ili waweze kufikishwa kwenye vyombo vya sheria,”alisema Wankyo.

 

Katika tukio jingine Said Athuman (32) Mkazi wa mkoa wa Tanga amekamatwa kwa tuhuma za kukutwa na matairi ya pikipiki 100 na 75 ya bajaji ambayo yanadhaniwa kuwa hayakulipiwa ushuru.

Alieleza, tukio hilo lilitokea septemba 21 mwaka huu majira ya saa 3:00 usiku eneo la Round About kata ya Dunda tarafa ya Mwambao wilaya ya Bagamoyo.

 

Wankyo alifafanua ,mtuhumiwa huyo alikuwa akitumia gari aina ya Mazda Pick Up yenye namba T 135 DPU ambapo gari hilo lilikamatwa wakati polisi wakiwa doria na inadhaniwa mali hizo zilipitia kwenye bandari bubu zilizopo Bagamoyo.

 

Pia mkazi wa Lugoba Mtupe Abdala (45) anashikiliwa kwa tuhuma za kusafirishama mbao ngumu 60 kwa kutumia gari lake aina ya Howo lenye namba za usajili T 693 CEH/T 672 DSK bila ya kuwa na kibali.

 

Hata hivyo ,Wankyo alielezea polisi walimkamata mtuhumiwa septemba 20 eneo la Chalinze Mzee tarafa ya Chalinze wilaya ya Kipolisi Chalinze katika mskao unaoendelea wa usiku na mchana wa kukamata wahalifu.

Comments are closed.