The House of Favourite Newspapers

Mbunge Ataja Sifa Za Mwanaume Wa Kumuoa

Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Geita, Upendo Furaha Peneza (Chadema).

Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Geita, Upendo Furaha Peneza (Chadema), ametaja sifa za mwanaume wa aina gani anayemhitaji maishani mwake amuoe, Amani linakupa zaidi. Upendo alifunguka hayo hivi karibuni ndani ya ofisi za gazeti hili namba moja kwa habari za ndani za maisha ya watu maarufu, Sinza Mori jijini Dar, alipokuwa akifanya mahojiano mambo mbalimbali yahusuyo kazi na maisha kwa ujumla.

 

Katika kipengele cha maisha, Upendo ambaye kwa muonekano ni mrembo wa haja, alisema kwa sasa hana mpenzi, mchumba wala mwanaume yeyote. Alisema katika maisha yake anapenda sana mwanaume mpambanaji na mwenye kujituma katika kusaka mafanikio maishani bila kujali rangi, kabila wala dini.

 

Mbunge huyo kijana ambaye mwishoni mwa wiki iliyopita alitawala vyombo mbalimbali vya habari, ikiwemo mitandao ya kijamii kufuatia mkutano wake na waandishi wa habari akiponda vibaya kitendo cha wanasiasa kuhama vyama, hakutaka kuingia kwa undani sana katika maisha yake ya kimapenzi ingawa alikiri kuwahi kupitia maisha ya uhusiano kama binadamu mtimilifu na kwamba kwa sasa anamuomba sana Mungu ampe mwanaume wa haja yake ili kutimiza furaha maishani mwake.

 

“Sina chochote kwa maana ya mpenzi, mchumba au mwanaume wa aina yeyote na mara nyingi sana huwa sipendi kuzungumzia maisha yangu binafsi, lakini kikubwa napenda sana mwanaume mwenye kujituma kutafuta mafanikio na kwa kweli namuomba sana Mungu atimize haja ya moyo wangu ili niweze kufurahia maisha, unajua ukiwa na mwanaume mchakarikaji na wewe unahamasika kupambana zaidi na maisha,” alisema Peneza.

 

Kuhusu kupigania maendeleo kwa vijana, Peneza alisema amekuwa akijitolea kuhakikisha vijana wanapewa haki sawa katika shughuli za uzalishaji na kutolea mfano namna ambavyo ametetea vijana kupewa nafasi za uchimbaji madini hususan katika Mkoa wa Geita. Pia, aliweka wazi namna anavyojipanga kuwasilisha hoja binafsi bungeni mwakani (Januari) ya kuitaka serikali itoe bure vifaa vya wasichana kuvaa wakati wa hedhi (sanitary pads) kwa ngazi za msingi na sekondari, kampeni ambayo anaamini ikifanikiwa itakuwa na manufaa kwa watoto wa kike ambao wakati mwingine hushindwa kumudu gharama.

Stori: Brighton Masalu, Amani

Comments are closed.