Baadhi ya wanafunzi waliosoma katika Shule ya Sekondari Mlalo iliyopo katika Kijiji Cha Mlalo, Wilayani Lushoto Mkoani Tanga, wamemfanyia ‘surprize’ aliyekuwa mwanzilishi wa shule hiyo na mwalimu mkuu, Sufian Shekoloa kwa kumuandalia tuzo pamoja na zawadi mbalimbali.
Tukio hilo la kihistoria lilifanyika tarehe 9, Desemba, 2018 katika bustani ya Hoteli ya kisasa ya The Atriums iliyopo Sinza Afrikasana jijini Dar na kuhudhuriwa na wanafunzi mbalimbali huku Mbunge wa Jimbo la Mlalo, Rashidi Shangazi akiwa mmoja wa wageni waalikwa.
Katika halfa hiyo, wanafunzi hao kwa kutambua mchango wa Mwalimu Shekoloa katika sekta ya elimu nchini na kwenye mafanikio yao, walimtunuku cheti cha shukurani, ‘Certificate of Appreciation’, Tuzo kubwa yenye muonekano wa ramani ya Tanzania, zawadi ya maboksi 17 ya ‘tailiz’ za kisasa pamoja pesa taslim.
Akiikabidhi tuzo hiyo, Shangazi kwanza aliwashukuru wanafunzi waliokuja na wazo hilo na kusema ni jambo litakalokuwa limeandika historia.
“Niwapongeze sana kwa hiki ambacho mmemfanyia leo Mwalimu Shekoloa, hakika yeye ni shujaa wa elimu Mlalo na Tanzania kwa ujumla. Historia yake imesheheni changamoto za kimaisha, uthubutu uliojaa ujasiri, utu na uchamungu wa kweli, upendo wa dhati kwa Usambara na wana Usambara wanyonge waliokosa fursa ya kupata elimu kwa kukosa kipato. Mwenyezi Mungu amjaalie na ambariki Mzee wetu ili aweze kuvuna japo matunda kidogo kwa sisi tuliopita katika mikono yake,” alisema Shangazi.
Naye Mwalimu Shekoloa alisema: “Sijui niseme nini kueleza furaha niliyonayo. Nimefarijika sana, zaidi ya sana. Nimefanya kazi hii ya ualimu kwa miaka zaidi ya 40 katika maeneo mbalimbali lakini sijawahi kufanyiwa kitu kama hiki. Mmeonesha kunijali sana. Mungu awabariki sana katika kazi zenu mnazofanya.”
Akizungumzia lengo hasa la kilichofanyika, mwenyekiti wa muda wa Umoja wa Wanafunzi Waliosoma Mlalo (MFOSA), Amran Kaima alisema kuwa, waliamua kumuandalia mwalimu huyo hafla hiyo baada ya kubaini kuwa mchango wake kwenye elimu ni mkubwa sana na alistahili tuzo.
“Hakika tuliopita kwenye mikono ya Mwalimu Shekoloa ni wengi sana na tumefanikiwa kwa sababu yake. Tukaona kuendelea kumsifia tu kwamba ana mchango katika maisha yetu bila kumfanyia chochote, siyo sawa. Ndiyo maana tukaamua kumtunuku tuzo na kumpa zawadi pia,” alisema Kaima.
Akawataja waliofanikisha tukio hilo kuwa ni Mariam Hozza, Jamila Juma, Salmina Shemdoe, Neema Mauya, Shufaa Hozza, Saumu Mbwambo, Ashura Mhando, Bius Kigae, Fatuma Mwekijazi, Fatuma Wakanai, Salome Kisu, Pilli Hizza, Mwanasha Nyangasa, Rahima Mdoe, Mariam Malenge, Amina Kiduma, Fatuma Shangazi na Sikudhani Gilla.
Wengine ni Hassan Gilla, Rashidi Semboga, Mohammed Mdoe, Sefu Kaima, Yusuph Shemweta, Nicolaus Rupia, Shaban Ahmed, Salim Hozza, Omary Hozza, Hassan Twalibu, Amran Kaima, Ally Yusuph, Rashidi Mashina na Itikija Msuya.
Comments are closed.