MBUNGE wa Jimbo la Kibiti mkoani Pwani, Twaha Mpembenwe amepata nguvu ya kurudi jimboni kwake kuwashukuru wapiga kura wake wa Kijiji cha Mtunda kufuatia mambo makubwa aliyowafanyia ndani ya kipindi kifupi kisichozidi mwaka mmoja tangu walipomchagua.
Mpembenwe akiwa kijiji cha Mtunda aliwaeleza wananchi hao jinsi alivyofanikisha kuwasaidia mambo mbalimbali ndani ya kipindi chake kifupi kama mbunge wao.
Mbunge huyo aliwaeleza jinsi alivyofanikisha kugawa vifaa vya ujenzi ikiwemo mifuko ya saruji zaidi ya 1500, tani moja ya nondo na mabati kwa ajili ya kukamilisha ujenzi vituo vya afya vya kisasa, shule za kisasa, kompyuta mashuleni na vinginevyo kwenye jimbo hilo ikiwemo kijiji hicho.
“Sitaki mama zangu muendelee kuhangaika kutafuta sehemu salama kwa ajili ya kwenda kujifungulia na matibabu mengine ndani ya kijiji hiki cha Mtunda na sitaki wanafunzi wasomee madarasa mabovu yenye kuta mbovu ambazo zingine kama zinauliza, niue nisiue?
“Nataka tuwe na shule bora ili ufaulu wetu uwe wa juu na sifuri kwenye mitihani ya taifa ibaki kuwa historia iliyopita kijiji hapa.
“Mama zangu najua mlikuwa na tatizo kubwa la kituo cha afya lakini hilo nalo litabaki kuwa historia katika Kijiji cha Mtunda”, alisema Mbunge Mpembenwe.
Mbunge huyo amewaambia wananchi hao kuwa pamoja na misaada hiyo anafahamu tatizo lingine kwenye kijiji hicho ni upatikanaji wa maji safi na salama.
“Mama zangu na baba zangu shida ya upatikanaji wa maji kwenye kijiji hiki naijua vizuri sana na hivi tunavyoongea nimeshawashirikisha jamaa zangu kutoka nje ya nchi ambao wamenielewa na hivi tunavyoongea tayari wakandarasi wameshaanza kazi hapa kijijini nafikiri wenyewe mnawaona.
“Najua mama zangu na baba zangu kijiji hiki suala la maji limekuwa tatizo sugu na limeshasababisha matatizo mengi ikiwemo ndoa nyingi kuvunjika, maana unakuta mama anakwenda kutafuta maji na kukaa huko masaa kibao akirudi nyumbani baba anachachamaa ndoa zinavunjika.
“Tatizo la maji hapa kijijini nalo linakwenda kukoma kabisa muda mfupi ujao” Nani kaka Mpembenweeee? Aliwauliza Mbunge huyo.
Baada ya kueleza hayo Mpembenwe aliwaeleza wananchi hao jinsi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan alivyowasaidia wakazi wa Kibiti katika suala la maendeleo.
Akielezea baadhi ya mambo makubwa aliyoyafanya Mama Samia kwa wakazi hao Mpembenwe amesema ametoa fedha nyingi na misaada mbalimbali ya kimaendeleo ya Kibiti na kuboresha sekta za elimu, afya na mengineyo.
Jamani nani kama Mama Samia? Hakuuunaaaa…. Ndivyo walivyosikika wakijibu wanakijiji hao. Baada ya kuwashukuru wakazi wa kijiji hicho ziara hiyo iliendelea kijiji cha Mjawa kilichopo Jaribu Mpakani.
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS NA ISSA MNALLY /GPL