The House of Favourite Newspapers

Mfaransa Abadili Mbinu za Ubingwa Simba

KOCHA Mkuu wa Simba, Mfaransa, Pierre Lechantre, anataka kubadili mbinu za kuhakikisha anachukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu bila ya kikwazo cha aina yoyote.

Simba ambayo kwa sasa inaongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 42, imeizidi Yanga iliyo nafasi ya pili kwa pointi tano pekee, jambo ambalo limeongeza presha kwao katika mbio za kuwania ubingwa.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Mfaransa huyo alisema katika hilo, atahakikisha anabadili uwanja wa kufanyia mazoezi ambapo kwa sasa anataka wawe wanajificha bila ya kuonekana na watu tofautitofauti.

“Tunapokuwa mazoezini huwa nawapa mbinu nyingi wachezaji wangu ikiwemo jinsi ya kupiga pasi, upigaji wa kona au faulo.

“Sasa tunapofanya mazoezi hayo sehemu ya wazi na kila mmoja, hilo linakuwa ni tatizo kubwa, nahitaji tuwe tunafanya mazoezi yasiyo ya wazi ili nikitoa maelekezo yasionwe na mtu asiyehusika na timu.

“Watu wanapoona mazoezini mnachokifanya, ikija kwenye mechi wanajua nini kinaenda kufanyika ikitokea kama mmepata kona au faulo,” alisema Lechantre.

Ikumbukwe kuwa, tangu Mfaransa huyo achukue mikoba ya kuinoa Simba mapema mwaka huu, timu hiyo imekuwa ikifanya mazoezi yake kwenye viwanja tofauti ikiwemo Bandari, Uhuru na Boko ambako watu mbalimbali wanahudhuria wakiwa mashabiki wa timu tofauti.

 

Na Omary Mdose na Ibrahim Mussa.

Comments are closed.