The House of Favourite Newspapers

Mhadhiri Makerere Agomea Dhamana, Ataka Museveni Afike Mahakamani

MHADHIRI katika idara ya utafiti ya Chuo Kikuu cha Makerere, Uganda, Dr Stella Nyanzi, ameitaka mahakama ya Buganda Road Court kumwita Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, kuhusiana na madai kwamba mhadhiri huyo alimdhalilisha (Museveni) kwa kumtukania mama  yake marehemu katika mtandao wa Facebook.

Dr Nyanzi anayekabiliwa na  mashitaka ya matumizi ya lugha mbaya katika mawasiliano, aliiambia mahakama hiyo jana kwamba Museveni lazima afike mahakamani hapo kueleza alivyochukizwa na  ujumbe wake alioweka kwenye mtandao huo.

“Polisi wakamilishe uchunguzi katika muda mfupi iwezekanavyo na wamlete Rais Museveni mahakamani aeleze alivyochukizwa na ujumbe wangu,” alisema Nyanzi.

Dr Nyanzi amekana mashitaka hayo, na hakuomba dhamana kama ilivyotegemewa ambapo alirejeshwa rumande katika Gereza la Luzira hadi Novemba 22 mwaka huu atakapofikishwa mahakamani tena.

Kwa mujibu wa serikali inayoendesha kesi hiyo, inadaiwa Septemba 16 na 19, 2018, Dr Nyanzi  aliandika katika ukurasa wake wa Facebook maneno ya kumtusi hayati Ester Kokundeka, aliyekuwa mama wa rais huyo.

Inadaiwa Nyanzi aliendelea kutuma ujumbe mbalimbali wa nia ya kuvuruga amani, utulivu na haki ya mambo ya faragha ya rais huyo.

 

Comments are closed.