The House of Favourite Newspapers

Michirizi Ya Damu – 11

0

“Ni mambo makubwa yaliyonitokea. Hakika nitamchukia Keith maisha yangu yote,” alisema Fareed huku akimwangalia Asteria.

“Kuna nini tena?”

Hapo ndipo Fareed alipoanza kusimulia kila kitu kilichokuwa kimetokea. Asteria alikuwa kimya akimsikiliza, mambo aliyokuwa akimwambia yalimuumiza mno, wakati mwingine machozi yalikuwa yakimlenga mpaka kumtoka machoni mwake, aliumia, hakuamini kama Fareed alikuwa amepitia mambo kama hayo.

Hakuamini kama Keith, yule mwanaume aliyekuwa na pesa, aliyekuwa na uwezo wa kufanya kitu chochote kile ndiye ambaye angefanya mambo hayo yote, yalitisha, na hata Fareed aliposema kwamba ni lazima arudishe kisasi, kwake hakukuwa na utetezi, alimfanyia mambo mabaya, hivyo akamuunga mkono.

“Ninakuunga mkono! Chochote utakachoamua, sawa tu,” alisema Asteria.

Huo ndiyo uamuzi aliokuwa amefikia, hakutaka kubaki hivyohivyo, moyo wake ulimuuma mno na hakutaka kukubali hata mara moja, alitaka kumuua mwanaume huyo kwa kuamini kwamba moyo wake ungekuwa na amani tele.

Hakutaka kuwasiliana naye, hakutaka kumpigia simu, aliamini kwamba Keith alijua kwamba alikufa, hivyo alichokifanya ni kubaki kimya ili kuamuacha aendelee kuhisi kwamba tayari alikuwa amekufa kule baharini.

“Nitamuua tu! Tena kwa mkono wangu,” alisema Fareed huku moyo wake ukiwa kwenye maumivu makali.

***

Maria alikichanganya kichwa cha Keith, hakutaka kukubali hata mara moja, kwake, msichana huyo alionekana kuwa na uzuri wa ajabu na alipanga kuwa naye maisha yake yote, hata kama ingemgharimu kiasi cha fedha kikubwa namna gani lakini ilikuwa ni lazima amchukue.

Walipoondoka Malaysia safari ya kwanza ilikuwa ni kwenda nchini Marekani. Hakutaka kumuacha msichana huyo, alizungumza naye sana, alimtongoza, kwa kutumia uwezo wake kifedha, akafanikiwa kumpata msichana huyo ambaye alikubaliana naye kwenda nchini Marekani kula raha kama kawaida yake.

Huko, walifanya kila kitu kilichotakiwa kufanywa kwa wapenzi, akatumia kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya Maria. Akamtambulisha kwa marafiki zake, kwa kuwa alikuwa kwenye makwaruzano na mkewe kwa muda mrefu, akawaambia kwamba huyo ndiye ambaye angeziba pengo la mkewe kama tu wangetengana.

Maisha yaliendelea kama kawaida, hakutaka kumkumbuka Fareed, aliamini kwamba msichana huyo alifariki dunia nchini Dubai, moyo wake ulijisikia amani tele, kuua, halikuwa jambo la kushangaza kwake, kama walivyokuwa mabilionea wengine, hata kwake kuua ilikuwa ni sawa na kumuua panzi.

Uhusiano wao haukuwa siri hata kidogo, waandishi wa habari wakazipata taarifa hizo, wakaanza kuwapiga picha na kuziweka kwenye mitandao huku wengine wakizitumia picha hizo kuziweka katika magazeti yao.

Kila mmoja alishtuka, hakukuwa na aliyeamini kama mzee huyo angemchukua msichana kama Maria. Si kwamba hakuwa mzuri bali alikuwa msichana wa Kiafrika, na mabilionea wengi nchini Marekani walipenda kuwa na Wazungu wenzao.

Safari hazikukoma, mara kwa mara walikuwa wakisafiri huku na kule wakila bata, hakutaka kuona akitulia, kwa sababu alimpenda Maria kwa mapenzi ya dhati aliamini kwamba kama angekwenda naye sehemu mbalimbali kula raha basi ingemfanya kufanikiwa kuliteka penzi la msichana huyo moja kwa moja.

Kwa kuwa alijua kwamba alikuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi na bilionea mkubwa duniani, Maria hakutaka kuona mwanaume huyo akiondoka mikononi mwake, alijitahidi kumfanyai utundu mkubwa kitandani kiasi kwamba mzee wa watu alichanganyikiwa kabisa.

Alimfanyia utundu mithili ya mwanamke aliyetoka kuchezwa siku za karibuni, alijua kummiliki mwanaume, alimfanyia mambo mengi ambayo mengine mzee huyo hakuwahi kufanyiwa, alibaki akistaajabu kwamba msichana kama Maria aliwezaje kumfanyia mambo yote hayo.

“How did you know all these things?” (umejuaje mambo yote haya?) aliuliza Keith huku akiwa amelala pembeni mtupu, kijasho kilikuwa kikitoka, kwa shughuli aliyokuwa ameonyeshewa, hata kuendelea alishindwa.

“I was taught to take care of men like you!” (nilifundishwa kuwashughulikia wanaume kama wewe) alisema Maria.

“Ooh! Maria, I will never leave you, just be with me forever,” (Ooh! Maria, sitokuacha kamwe, naomba uwe nami milele yote) alisema Keith.

“No problem! Give me some more sweetie,” (hakuna tatizo! Naomba tena mpenzi) alisema Maria, wakati akiyazungumza hayo tayari alikuwa juu ya Keith na kumkalia, akaanza kumminyaminya mwili wake.

“I can’t! You will kill me,” (siwezi! Utaniua) alisema mzee huyo.

“You rather die. Give me some more,” (Bora ufe. Naomba tena) alisema Maria, kilichofuata ni kushika maiki na kuanza kuimba.

Hiyo ndiyo ilikuwa njia sahihi ya kumteka mzee huyo, kwa kufanya hivyo, alizidi kupendwa, alipewa kiasi kikubwa cha fedha kilichomchanganya kupita kawaida, hakutaka kuona akimuacha mwanaume huyo, kwake, alikuwa kila kitu na alitaka kuhakikisha anazichuma pesa zake kadiri anavtyoweza.

Mzee wa watu alizidi kupagawa, alikuwa radhi kugombana na kila mtu lakini si Maria. Alimpenda kwa penzi la dhati na kila siku alikuwa akipewa mambo mapya kitandani ambayo yaliuchanganya moyo wake kupita kawaida. Hakutaka kuwaambia marafiki zake kuhusu Maria, alijua fika kwamba kulikuwa na kugeukana, siri ya ujuzi wa Maria kitandani ukabaki moyoni mwake, aliendelea kulala naye na kufanyiwa vituko vya kimahaba kila siku.

“Nitampa kila kitu! Hakika ameniondoa ukungu katika mapenzi kitandani! Mwanamke anajua utadhani nini! Ni lazima nitangaze ndoa,” alisema Keith huku akionekana kumaanisha alichokuwa akikiongea.

***

Fareed alikuwa safari akielekea nchini Kuwait, tayari aliwasiliana na bilionea Sadiq Rahman kutoka nchini humo ambaye alikuwa akimuhitaji kimapenzi kuliko kitu chochote kile. Moyo wake ulikuwa na furaha na muda wote alikuwa akimshukuru Asteria kwani yeye ndiye alikuwa mchakarikaji katika kuwatafutia mabwana waliokuwa na pesa katika nchi za Kiarabu.

Njiani, huku akiwa ndani ya ndege moyo wake ulikuwa na hofu tele, hakujua nu kitu gani ambacho kingetokea huko. Hakutaka kuona Keith akigundua kwamba alikuwa hai, alitaka mwanaume huyo ajue kwamba alikuwa amekufa mpaka siku ambayoo angeamua kumuua kama kulipa kisasi.

Akiwa ndani ya ndege, akachukua Gazeti la The Mirror na kuanza kulisoma. Humo ndania akakutana na habari iliyomshtua ambayo ilimuhusu bilionea Keith ambaye alikuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi na msichana wa Kinigeria aliyeitwa Maria.

Moyo wake ulimuuma sana, wivu ukamkamata, japokuwa alifanyiwa mambo mengi mabaya na mwanaume huyo lakini bado sehemu ya moyo wake ulikuwa ukimpenda. Akakunja sura yake na kuliweka pembeni gazeti lile.

Safari ilikuwa ndefu lakini walifika salama ambapo akateremka na nje akakutana na mwanaume mmoja aliyekuwa na boksi kubwa kiasi lililoandikwa jina lake alilokuwa akijulikana sana kipindi hicho, Farida.

Akamsogelea mwanaume huyo na kisha kumsalimia. Kwa kuwangalia, ilikuwa vigumu kugundua kwamba mtu huyo alikuwa mwanaume, alijipamba, alijiwekea wigi kichwani, alivalia gauni huku midomo yake ikiwa imepakwa shedo iliyokolea na nyusi alizinyoa kisha kupaka wanja.

Alivutia, kwa nyuma, alikuwa na mzigo wa maana, kifua kilituna, alikuwa na muonekano wa kike kwa asilimia mia moja na kila mwanaume aliyemwangalia, alimtamani.

Akachukuliwa na mwanaume huyo na kuelekea ndani ya gari na kuanza safari ya kuelekea katika jumba alilotakiwa kulala kwa siku hiyo. Njiani, macho yake yalikuwa yakiangalia huku na kule, moyo wake ulichanganyikiwa kwa furaha, haikuwa mara yake ya kwanza kufika nchini humo ila kilichomfanya kuwa na furaha ni kwamba alirudi kwenye chati baada ya kupotea.

Hawakuchukua muda mrefu wakafika katika jumba moja kubwa ambapo gari likaingizwa ndani. Akabaki akiliangalia jumba hilo, lilikuwa kubwa, lenye mapambo yaliyonakishiwa kwa rangi ya dhahabu, bwawa kubwa la kuogelea na vitu vingine vingi, kwa kifupi, kwa kuliangalia tu ilikuwa ni rahisi kugundua kwamba hilo lilikuwa jumba la bilionea mkubwa nchini hapo.

Akaingia ndani, macho yake hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule, lilipendeza sana, aliliguata kochi na kutulia, lilibonyea na kuyafanya makalio yake kuhisi yamekalia kitu kilichokuwa na thamani kubwa.

Wakati akiwa hapo, mlango mwingine ukafunguliwa na mwanaume mmoja aliyevalia msuli kutokea sebuleni hapo. Alikuwa mwanaume mwenye kitambi kikubwa, ndevu nyingi alizozipaka hina, alionekana kabisa kwamba alikuwa ndama, akamfuata Fareed kochini pale, akamuinua kisha kumkumbatia.

“Wewe ndiye mwenyewe?” aliuliza Mzee Sadiq.

“Ndiyo!”
“Aisee! Unaonekana kama mwanamke mbichi,” alisema Mzee Sadiq huku akiachia tabasamu.

Kwa mwendo wa madaha akamchukua na kumpeleka katika chumba walichotakiwa kulala usiku huo. Walipofika, akamuweka kitandani na kumwambia amsubiri kwani kulikuwa na mambo alitaka kukamilisha kabla ya kushinda naye chumbani.

“Haina shiida.”

Mzee huyo akatoka chumbani humo. Fareed alibaki akikishangaa chumba hicho, kilimstaajabu sana, na kila alipokuwa akikiangalia, aliona kabisa hakikuwa kikistahili kukaliwa na mtu kama yeye.

Wakati akiwa hapo, mara simu yake ikatoa mlio kumaanisha kulikuwa na ujumbe mfupi wa simu umeingia. Haraka sana akaichukua simu yake na kuufungua ujumbe huo ambao haukuandikwa maneno mengi, ulisomeka: ‘Nimekuona ukiingia Kuwait. Naomba nikuone ukitoka kwa huyo babu’ ulisomeka ujumbe huo, akashtuka.

“Wewe nani?” aliuliza.

“Naitwa Belleck Peter.”
“Ndiye nani?”

“Huwezi kunijua. Ila nilipata mawasiliano yako kutoka kwa Asteria. Amenipatia namba yako. Naomba nikuone ukitoka kwa huyo mzee,” aliandika mwanaume huyo.

“Mmh! Sawa.”
Hapohapo bila kuchelewa Fareed akampigia simu Asteria na kumuuliza kuhusu mwanaume huyo. Asteria alikiri kumpa namba kwa kuwa alikuwa mteja mkubwa wa wanaume tata. Alikuwa Mmarekani bilionea ambaye kwake, pesa hazikuwa tatizo hata kidogo.

“Ila hajuani na Keith! Asije kuniletea shida!”
“Hilo ondoa shaka. Hawajuani kabisa.”

“Sawa,” alisema Fareed na kukata simu. Hapohapo akapiga magoti, akamshukuru Mungu kwa kumuumba mwanaume, kwani kama angekuwa mwanamke, hakika asingeweza kukutana na mabilionea hao.

“Mungu! Nashukuru sana kwa kuniumba mwanaume. Ungeniumba mwanamke, sijui kama ningepata mazali kama haya,” alisema Fareed huku akitoa tabasamu pana.

***

Muda huo ulikuwa zamu ya Mzee Sadiq, alilala na Fareed usiku kucha, haikuishia siku hiyo, huo ulikuwa muda wake wa kuwa na mwanaume tata huyo. Maisha ya Fareed yaliendelea kubadilika, alikaribia kuwa milionea kwa sababu tu alijiuza kwa wanaume matajiri ambao walikuwa tayari kutoa kiasi chochote cha fedha mpaka kufanikisha kile walichokuwa wakikihitaji.

Siku ziliendelea kukatika, waliendelea kuwa pamoja. Japokuwa maisha yalikuwa mazuri, alipata kila kitu alichokuwa akikihitaji lakini hakuacha kuwasiliana na wanaume wengine, wote hao alitaka kulala naye na mwanaume ambaye alikuwa na hamu naye kwa kipindi hicho alikuwa Belleck.

Aliendelea kuwasiliana na mwanaume huyo, hakutaka kuonana naye kwa muda huo, alitaka kumuweka kiporo, alale naye katika siku za mwisho za kutaka kuondoka nchini humo.

Kwa kuwa mwanaume huyo alimuhitaji sana, alijitahidi kumtumia kiasi kikubwa cha fedha, kila shida ambayo Fareed alikuwa akiililia, alitumiwa fedha na mwanaume huyo ingawa hawakuwa wameonana.

Baada ya kukaa na Mzee Sadiq kwa siku kadhaa hatimaye akaamua kuondoka nyumbani kwa mzee huyo na kwenda kuonana na Belleck ambaye alionekana kuwa na kiasi kikubwa cha fedha.

Macho yake yalipotua kwa mwanaume huyo, moyo wake ulimlegea, alikuwa mwanaume mwenye sura nzuri, ya kitoto ambapo mwili wake ulikuwa umejazia kidogo. Alipomuona tu, moyo wake ukatokea kumpenda, alikuwa ana mvuto wa ajabu, zaidi ya wanaume wote ambao aliwahi kukutana nao.

Belleck alivalia suti iliyotengenezwa na Kampuni ya Pollo, alivalia saa nzuri, ya thamani iliyotengenezwa na Kampuni ya Solex, kwa kifupi, muonekano wake ulikuwa ni wa kitajiri.

“Fareed…” aliita Belleck huku akimwangalia mwanaume huyo.

“Nimekuja kukuona mpenzi!” alisema Fareed.

Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kuonana na mwanauume huyo, kilichofuata baada ya hapo ni kula maisha kwa kutembea sehemu mbalimbali. Fareed alijisikia amani moyoni, hakuuacha kumshukuru Mungu kwa kumuumba mwanaume.

Alijua kwamba kuulikuwa na wanawake wengi waliotamani nafasi kama ile aliyokuwa nayo lakini hakukuwa na yeyote aliywahi kuipata. Alifarijika na muda wote alijiona kuwa mtu mpya, aliyebarikiwa na Mungu, mtu msafi ambaye hata kama angekufa basi angekwenda peponi.

“Nakupenda sana Fareed,” alisema Belleck huku wakiwa kitandani.

“Nakupenda pia!” alijibu Fareed na kumbusu shavuni.

***

Belleck Peter alikuwa miongoni mwa matajiri wakubwa waliokuwa na kampuni nyingi nchini Marekani. Alikuwa miongoni mwa watu waliojitengenezea utajiri mkubwa huku ukiendelea kuongezeka kila siku iliyoitwa leo.

Alikuwa miongoni mwa mabilionea ambao waliheshimika nchini Marekani kutokana na mchango mkubwa aliokuwa akiutoa katika jamii. Utajiri wake wa dola bilioni kumi na tano ulikuwa ukitikisa kila kona. Alikuwa mtu wa watu, bilionea asiyekuwa na sifa, bilionea ambaye siku zote alitaka kuishi katika maisha ya chini kwa ajili ya kuwafanya hata wale masikini kuona wapo sawa naye.

Japokuwa alikuwa na kampuni nyingi lakini nyuma ya pazia utajiri wa mwanaume huyo ulikuwa ukisaidiwa na biashara kubwa ya madawa ya kulevya aliyokuwa akiifanya. Hiyo ilikuwa siri kubwa, aliwaandaa vijana wake ambao walikuwa wakizunguka dunia nzima kwa ajili ya kumfanyia kazi hiyo.

Alijificha kwa kutumia kivuli cha serikali, hakukuwa na mtu aliyehisi kama mwanaume huyo alikuwa akishughulika na biashara hiyo. Alikuwa na vijana wa Kimexico ambao walikuwa na kazi kubwa ya kusambaza mizigo yake Marekani ya Kati na Kusini, alikuwa na vija abarani Afrika ambao nao alikuwa akiwatumia kumsafirishia biashara yake.

Alitisha, utajiri wake uliongezeka. Kwa kuwatumia vijana wake, akawatafuta watu wengine ambao walikuwa na kazi ya kumeza dawa hizo na kuzipeleka sehemu husika. Wanaume wengi waliogopa kumeza kwa kuwa walipata tabu muda wa kutoa madawa hayo chooni kupitia sehemu ya haja ndogo na ndiyo ikawa sababu ya kuwatafuta wanaume waliokuwa wakijihusisha na mapenzi ya jinsi moja.

Kwenye kutafuta watu hao, aliwapata wengi, aliwatumia, hakutaka kuacha, aliendelea kujificha kwa mwamvuli wa serikali. Kwenye kuendelea kutafuta wanaume hao, ndipo akafanikiwa kumpata Fareed.

Hakumpenda mwanaume huyo, aliamua kuwa naye kwa kuwa alitaka kuona biashara yake ikiendelea kusonga mbele, alitaka kumtumia katika kusafirisha biashara zake kama walivyofanya wenzake.

Alitumia kiasi kikubwa cha fedha kumuhonga lakini alijua kwamba mwisho wa siku angepata kile alichokuwa akikihitaji. Alimuonyeshea mapenzi ya dhati, Fareed hakujua kwamba mwanaume huyo hakuwa tofauti na Keith, aliendelea kumwamini kila siku.

Aliwapanga vijana wake kama kawaida, ilikuwa ni lazima kumtumia mwanaume huyo kusafirisha madawa yake kupeleka nchini Ufaransa na baada ya kufika huko, vijana wake wangempokea na kumlazimisha kuyatoa kisha kumuua.

Hilo halikuwa tatizo, akajipanga kwa ajili ya kufanya kazi hiyo. Kabla ya kumsafirisha ilibidi kwanza amleweshe na kisha kumywesha kete za madawa ya kulevya na kisha kumlazimisha kusafiri kuelekea nchini Ufaransa.

“Ushawahi kunywa Kemikal Boom?” aliuliza Belleck huku akimwangalia mwanaume huyo.

“Hapana!”
“Hahaha! Unakosa utamu mkubwa sana. Ni pombe nzuri yenye kulewesha kidogo,” alisema Belleck huku akiifuata chupa moja iliyokuwa mezani ambayo iliandikwa Kemical Boom ambayo ilikuwa na kilevi cha 70%.

“Mmh! Nitaiweza?”
“Kwa nini uishindwe mpenzi! Ni tamu sana,” alisema Belleck huku akichukua glasi na kuimimina pombe ile katika glasi ile aliyokuwa nayo.

Ilikuwa vigumu kwa Fareed kugundua kwamba mwanaume huyo alikuwa mtu mbaya katika maisha yake, alichokiona, kilikuwa ni mapenzi ya dhati, kila alichokuwa akifanyiwa, kwake kilionekana kuwa sahihi kwa kuwa tu alipewa fedha nyingi na mwanaume huyo.

Akaifakamia pombe hiyo na kuanza kunywa kwa kasi. Hakuchukua dakika nyingi, akahisi viungo vya mwili wake vikianza kuuma, akaanza kusikia kizunguzungu, ilikuwa pombe kali na hakutakiwa kunywa nyingi kiasi hicho. Wakati akiwa kwenye hali hiyo, ndiyo kwanza Belleck alikuwa akicheka tu.

“Nimelewa…..” alisema  Fareed. Hakukaa kwenye hali hiyo kwa muda mrefu, akaona giza, akajilaza kitandani, alionekana kama mtu aliyepoteza fahamu.

“Safi sana! Ngoja niwaite vijana,” alisema Belleck, hapohapo akachukua simu na kuwapigia vijana wake wa kazi.

****

Ndani ya dakika kadhaa wanaume watatu wakafika mahali hapo, walikuwa wamejiandaa vilivyo, kwa jinsi walivyoonekana, walikuwa tayari kufanya kazi muda wowote ule. Belleck akawakaribisha huku akionekana kuwa na furaha tele, katika maisha yake yote, hakukuwa na kitu kilichokuwa kikimuingizia fedha kama biashara ya madawa ya kulevya.

Alitaka kumtumia Fareed katika biashara zake, alitaka kumpa mzigo wa madawa ya kulevya na kuyasafirisha maka nchini Ufaransa. Hilo kwake halikuwa tatizo, usiku huohuo wakamnywesha kete kumi na mbili za madawa ya kulevya na kumsubiri aamke ndipo wamwambie kuhusu safari hiyo kwani tayari walimuandalia tiketi yake.

Fareed aliamka baada ya saa moja kupita. Alijisikia uchovu, hakujua alikuwa mahali gani. Pale alipokuwa kulikuwa na kitanda kikubwa, chumba kizuri, akaamka na kuanza kuangalia huku na kule na ndipo kumbukumbu zake zikaanza kurudi na kukumbuka kwamba mara ya mwisho alikunywa pombe kali na baada ya hapo hakujua ni kitu gani kiliendelea.

“Nipo wapi? Belleck kanileta wapi?’ alijiuliza huku akisimama kutoka pale alipokuwa.

Akaelekea dirishani, akachungulia, alikuwa kwenye ghorofa ya nne, aliogopa, ile haikuwa hoteli aliyokuwa amefikia, ilikuwa nyingine kabisa. Alipoangalia kwenye kimeza kidogo akakutana na kitabu kidogo kilichoandikwa ‘King Caspian Hotel’.

“Nimefikaje King Caspian?” alijiuliza.

Aliijua hoteli hiyo, ilikuwa hapohapo Kuwait, haikuwa hoteli ile aliyofikia, alijiuliza sana lakini mwisho wa siku akajua kwamba Belleck ndiye aliyekuwa akifahamu kila kitu kilichokuwa kimetokea.

Alijaribu kutoka ndani ya chumba hicho, mlango ulikuwa umefungwa kwa nje, moyo wake ukajawa na hofu kwa kuhisi kwamba Belleck alikuwa mmoja wa wafanyakazi wa Keith ambao walijua kwamba hakuwa amekufa baharini hivyo kutaka kumuua tena.

“Mungu! Huyu Keith ananitakia nini lakini?” alijiuliza huku akionekana kuwa na hasira kali.

Akaliangalia begi lake lililokuwa pembeni, zipu ilikuwa wazi kuonyesha kwamba kulikuwa na mtu alilifungua, alipoangalia ndani, akakuta kukiwa kumepekuliwa, hakukuwa na vitambulisho vyake, hakukuwa na hati ya kusafiria.

Alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea. Moyo wake ukaingiwa na hofu kwa kuona kwamba alipoteza kila kitu, akakifuata kitanda, akakaa na kuanza kulia.

Wakati akiendelea kulia, mara mlango ukafunguliwa na wanaume watatu kuingia ndani ya chumba hicho. Hawakuzungumza kitu, walibaki wakimwangalia. Harakaharaka Fareed akasimama na kuwaangalia, akajua kwamba watu hao ndiyo waliokuwa wamefungua begi lake na kupekua.

“Naomba mnisamehe! Hivi kwa nini Keith anataka kuniua? Nimemfanya nini? Kama ni gharama za pesa yake nitamrudishia,” alisema Fareed huku akiendelea kulia.

“Keith ndiye nani?”
“Bosi wenu aliyewatuma!”
“Hatumfahamu huyo. Tumekuja kukupa ujumbe mmoja.”

“Upi?”
“Unatakiwa kusafiri leo kuelekea Ufaransa,” alisema mwanaume mmoja.

“Kuelekea Ufaransa?”
“Ndiyo!”
“Kufanya nini?”
“Una mzigo wetu tumboni mwako, utatakiwa kufika nchini humo. Utakapofika katika Jiji la Marseille, ukitoka nje utakuta kuna mtu anakusubiri huku akiwa na bango lililokuwa na jina lako, mfuate huyo, ukipinga na kufanya kitu cha tofauti, tutakuua!” alisema mwanaume huyo huku akimwangalia Fareed kwa macho yaliyomaanisha kile alichokuwa akikisema.

“Sawa,” alijibu Fareed huku akitetemeka.

Muda ulipofika, akakabidhiwa kila kitu na kuanza kuelekea uwanja wa ndege. Moyo wake ulijuta, wakati mwingine alijiapiza kutokurudia kufanya ukahaba kwa Wazungu kwani wao ndiyo waliokuwa wakimuingiza kwenye matatizo tofauti na Waarabu ambao wao walichokuwa wakikihitaji ni mapenzi tu.

Njia nzima alilia, hakunyamaza, mpaka alipoingia ndani ya ndege bado aliendelea kulia kama kawaida. Moyo wake ukaanza kuifikiria safari hiyo, hakujua kama angevuka salama uwanja wa ndege kwani kwa nchi za Ulaya na Marekani kulikuwa na ulinzi mkali viwanjani kuliko hata katika nchi za Afrika na Asia.

Alitumia saa thelathini kwenye ndege, tena kwa kubadilishabadilisha mpaka alipofika nchini Ufaransa katika Jiji la Marseille. Akateremka na abiria wengine, mabegi yakapita sehemu ya uchunguzi na wao kuruhusiwa.

Hakushtukiwa na mtu yeyote yule, akatoka na kwenda sehemu ya watu waliokuja kuwasubiri watu wengine, hapo akamuona kijana mmoja akiwa amesimama huku akiwa na bango dogo lililoandikwa jina lake ambapo akamfuata na kujitambulisha kwamba yeye ndiye alikuwa Fareed.

“Are you Fareed?” (wewe ndiye Fareed?) aliuliza jamaa huyo huku akishangaa.

“Yes!” (ndiyo)

“How? Are you a boy or girl?” (Kivipi? Wewe ni mvulana au msichana?)

“Hey! You are wasting my time. Take me where Am suppose to be,” (Hey! Unanipotezea muda. Nipeleke ninapotakiwa kuwa) alisema Fareed huku akionekana kuanza kukasirika.

Mwanaume huyo hakuongea kitu chochote lakini alionekana kuwa na maswali mengi kichwani mwake. Alikuwa akijiuliza kuhusu mtu aliyekwenda kumpokea, ilikuwa awe na jina la kiume na wakati alikuwa na muonekano wa kike? Alivalia gauni refu, kichwani alikuwa na wigi, alipaka wanja na lipstic, sasa ilikuwaje awe mwanaume?

Hakutaka kujiuliza maswali zaidi bali ni kukaa kimya na kuendelea kuendesha gari kuelekea katika sehemu ambayo alitakiwa kumpeleka mgeni huyo. Akiwa hapo njiani akamtumia meseji Belleck kwamba mgeni aliyetakiwa kufika, tayari alikuwa ndani ya gari

***

Belleck aliwaanda vijana wake kwa ajili ya kazi ya kuyatoa madawa ya kulevya kutoka tumboni mwa Fareed. Yalikuwa ni madawa yenye thamani kubwa ambayo yangemuingizia kiasi kikubwa cha fedha.

Kete za madawa hayo zilikuwa tumboni mwa Fareed, kwa kawaida alitakiwa kwenda kujisaidia ili kutoa kete hizo lakini Bellck hakutaka kuona hilo likifanyika na badala yake alihitaji mtu huyo apasuliwe tumbo na kutolewa madawa hayo.

Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, waliwahi kufanya kazi kama hiyo kipindi cha nyuma kwa watu wengi, kuua, kwa vijana hao lilionekana kuwa jambo dogo sana ambalo lilikuwa ni kama kumuua sisimizi kwa kumkanyaga.

Walijiandaa nyumbani, walimtuma mwenzao kwenda kumpokea Fareed uwanja wa ndege ili atakapofika basi kazi ya kumpasua tumbo ianze mara moja.

Belleck alivyotumiwa meseji kuambiwa kwamba mtu huyo aliwasili na alikuwa ndani ya gari, naye akawapigia simu vijana wake na kuwaambia kwamba mtu waliyeta kumpasua tumbo na kumtoa madawa hayo alikuwa garini akielekea hapo nyumbani.

“Hakikisheni mnamuua na kutoa huo mzigo. Ni wa gharama sana, kama ukipotea nitapata sana hasara,” alisema Belleck kwenye simu.

“Hakuna shida mkuu! Wapo njiani wanakuja.”
“Basi haina shida. Kazi njema.”
“Nawe pia.”

****

Hawakuchukua muda mrefu wakafika ndani ya jumba hilo la kifahari. Moyo wa Fareed ulikuwa ukitetemeka, hakuamini kama kweli alikuwa amenusurika katika mdomo wa kifo kwa bilionea Keith lakini mwisho wa siku alikuwa kwenye mdomo wa kifo kwa bilionea mwingine.

Aliumia na wakati mwingine alikuwa akijutia kazi yake ya kujiuza aliyokuwa akiifanya kwa moyo mmoja. Aliwachukia Wazungu, hakutaka uswahiba nao tena, kila alipoifikiria safari ya maisha yake mpaka kunasa kwa watu hao, moyo wake uliumia kupita kawaida.

Gari likasimama katika eneo la kupaki magari na wanaume wawili waliokuwa na bastola kutokea mahali hapo. Wakaufungua mlango na kumshusha Fareed kinguvu kisha kuanza kumpeleka ndani.

Walimshangaa mwanaume huyo, muonekano wake ukawatia hofu kwa kuhisi kwamba huyo hakuwa mwanaume kama walivyoambiwa, walihisi kwamba alikuwa mwanamke kutokana na muonekano wake wa kike aliokuwa nao.

Wakamchukua na kumpeleka katika chumba kimoja kilichokuwa na meza kubwa pamoja na vifaa vya kumfanyia mtu upasuaji. Fareed alipoviona vifaa hivyo na chumba hicho, moyo wake ulimuuma mno, hakuamini kama siku hiyo na yeye alibebeshwa madawa ya kulevya kama walivyokuwa wakifanyishwa watu wengine.

“Call Dr. Watson,” (mpigie simu daktari Watson) alisema mwanaume mmoja.

Bonny Watson alikuwa daktari kutoka katika Hospitali ya St. Napoleon iliyokuwa hapohapo Marseille nchini Ufaransa. Daktari huyu ndiye aliyekuwa akitumiwa sana na Bilionea Belleck kwa ajili ya kuwafanyia upasuaji watu wote waliokuwa wakimeza kete za madawa ya kulevya nchini Ufaransa.

Hakukuwa na mtu aliyepona, wote waliokuwa wakipelekwa huko, walichomwa sindano ya usingizi na kufanyiwa upasuaji huo ambao uliwapelekea vifo vyao.

Alizoea kazi hiyo, alilipwa kiasi kikubwa cha fedha na hakutaka kuiacha. Mara kwa mara Bilionea Belleck alipokuwa akiwatuma watu, alipigiwa simu na kuambiwa aelekee nyumbani kwa bilionea huyo kisha kufanya kazi hiyo au kama alibanwa sana basi ilikuwa ni lazima mtu huyo apelekwe katika hospitali yake na kumfanyia upasuaji.

Muda huo alipigiwa simu na kijana wa Belleck na kumwambia kwamba kulikuwa na kazi alitakiwa kuifanya. Hakushtuka lakini kwa siku hiyo kulikuwa na ugumu kwani hospitalini hapo alikuwa na wagonjwa ambao walihitaji sana kufanyiwa upasuaji.

“Mleteni lakini nitamfanyia baada ya saa tano,” alisema Dk. Watson.

“Haina shida.”

Leave A Reply