The House of Favourite Newspapers

Mke wa kukupanda kichwani wa kazi gani

UKWELI ni kwamba, wapo wanaume ambao wako kwenye ndoa lakini hawana amani kabisa. Wanatamani kutoka lakini haiwezekani, wanabaki kuugulia. Hii ni kwa sababu wameoa wanawake wenye tabia ambazo hazifai.  Leo kupitia ukurasa huu nitakupa tabia ambazo wanawake pasua kichwa kwa waume zao wanazo. Anakupanda kichwani Mwanaume siku zote atabaki kuwa kiongozi wa familia lakini wapo baadhi ya wanawake hawataki kukubaliana katika hilo.

Wengi wanalazimisha usawa na wengine wakitaka wao ndiyo wawe na sauti kuliko waume zao. Hili nalo ni janga! Yaani mkeo anataka kila linalofanyika yeye awe mtu wa kutoa maamuzi! Kwa maana nyingine amekupanda kichwani, mke wa dizaini hii wa kazi gani?

Haridhiki na penzi Wapo wanawake ambao wewe unaweza kujitahidi kumpatia mapenzi kadiri unavyoweza lakini yeye hatosheki. Anakuchukulia wewe ni dhaifu sana na wakati mwingine kuhisi yupo mwingine anayeweza kumpa zaidi ya kile unachompa, huyu ni tatizo.

Wivu kupindukia Hatukatai, wivu ni muhimu sana kwenye suala la mapenzi lakini kuna ule wivu uliopindukia kiasi cha kuwa kero. Walio kwenye ndoa wananielewa namaanisha nini. Kwa kifupi mtu mwenye mapenzi ya dhati na mwenziye lazima awe na wivu lakini ukiwa na ule wa kupinduki ni tatizo linaloweza kuitibua ndoa.

Anahisi unamsaliti Huku kunatokana na kutokujiamini tu. Ukioa mwanamke ambaye kila wakati unapokuwa mbali naye anahisi unamsaliti, huyo hakuamini na kamwe hamuwezi kudumu. Mara kadhaa mtakuwa mkigombana akihisi una mwingine kumbe hakuna ukweli katika hilo.

Anahisi kaingia ‘cha kike’ Wapo wanawake ambao wanapoingia kwenye ndoa baada ya muda wanahisi wamekosea kuolewa na mwanaume huyo. Unakuta mke wa mtu anahisi fulani ambaye zamani alikuwa kwenye uhusiano naye angekuwa sahihi zaidi baada ya kuona upungufu fulani kwa huyo aliyemuoa.

Yuko kimasilahi Kuna wanawake ambao ukiwaoa wanakuwa na furaha na wewe ukiwa unazo tu, ukiishiwa wanaanza kununa na kuleta visirani vya hapa na pale. Hawa ni tatizo, mwanamke wa kweli ni yule anayeridhika kuwa na wewe kwenye shida na raha.

Yuko tayari muachane Hivi hujawahi kumsikia mke wa mtu akimwambia mumewe; ‘Kama vipi tuachane, kwanza kwetu sijafukuzwa na nilikuwa nakula, nalala, navaa.” Mwanamke anayeweza kumtamkia mume wake maneno haya, huyo si mke na kamwe hawezi kukufanya uwe na furaha.

Anajali yeye tu Siku zote wawili waliotokea kupendana wakioana wanakuwa mwili mmoja hivyo lazima watakuwa wanawaza na kufanya maamuzi pamoja. Ogopa sana mwanamke anayependa kutumia kipato chake kufanya mambo binafsi tena kwa siri. Kwa mfano kusaidia kwao, kujenga nyumba kwao, kuanzisha miradi yake bila kukushirikisha

Comments are closed.