The House of Favourite Newspapers

Mo Apata Msaidizi Simba

Mohammed Dewji ‘Mo’

WAKATI kikosi cha Simba kikijiandaa na mechi zake za kimataifa za Ligi ya Mabingwa Afrika, wachezaji wa timu hiyo sasa washindwe wenyewe tu.

Hiyo ni kwa kuwa baadhi ya mashabiki wa timu hiyo wameamua kujitokeza kuusaidia uongozi wa klabu hiyo uliopo chini ya mwekezaji mkuu wa klabu hiyo, Mohammed Dewji ‘Mo’ kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri katika mechi zake za Hatua ya Makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Mashabiki hao kupitia makundi yao mbalimbali ya mitandao ya kijamii kwa pamoja wamejitolea kushirikiana na uongozi wa timu hiyo kuwaongezea morali wachezaji hao ili kuhakikisha wanapambana vilivyo uwanjani katika mechi zao zote sita za makundi.

 

Habari za kuaminika ambazo Championi Ijumaa limezipata kutoka ndani ya Simba zimedai kuwa mashabiki hao kwa pamoja wamejipanga kuisaidia timu hiyo kiasi cha Sh milioni 150. Katika hatua hiyo ya makundi, Simba imepangwa kundi moja na timu za Al Ahly ya Misri, AS Vita Club ya DR Congo pamoja na JS Saoura ya Algeria ambayo itapambana nayo Januari 12, mwaka huu.

 

Fedha hizo zitatumika kwa ajili ya bonasi za wachezaji katika mechi zote sita, imeelezwa kuwa kila mechi wachezaji watakuwa wakipewa bonasi ya Sh milioni 25.

 

“Tayari harakati za kutafuta fedha hizo zimeshaaanza na ni matumaini yetu kuwa lengo hilo litatimia kwani tunataka mafanikio kwa hiyo ni lazima tujitolee. “Kwa hiyo, endapo tutafanikiwa kutoa kiasi hicho cha Sh milioni 150 basi uongozi nao utatoa kitita cha Sh milioni 150 nyingine kwa ajili ya bonasi za wachezaji na tumeshazungumza uongozi juu ya hilo,” kilisema chanzo hicho cha habari.

 

Alipoulizwa kuhusiana na hilo, Mratibu wa Simba, Abbas Ally alisema: “Mipango ya kuwaongezea motisha wachezaji wetu ili kuhakikisha tunafanya vizuri ipo, ila kuhusiana na mashabiki kuchangishana kwa ajili ya timu kusema kweli silijui.”

Comments are closed.