The House of Favourite Newspapers

Mrundi Aliyewavuruga Simba, Afichua Siri

KIUNGO wa Stand United, Mrundi, Bigirimana Blaise, amefichua siri ya bao lake la kusawazisha katika mchezo dhidi ya Simba kuwa limetokana na ahadi kubwa ya pesa waliyopewa na viongozi wao kabla ya mchezo huo.

Mchezo huo uliopigwa juzi Ijumaa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar ulimalizika kwa sare ya mabao 3-3 huku mchezaji huyo akifunga bao la kusawazisha na alitolewa nje mara baada ya bao hilo kufuatia kuumia mguu wake wa kushoto.

 

Simba imebaki kileleni na pointi 46, baada kucheza michezo 20 huku Yanga wakiwa nafasi ya pili na pointi 40 na ikiwa na mchezo mmoja mkononi kufuatia kucheza mechi 19.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Blaise alisema kuwa kabla ya mchezo huo walipewa ahadi ya kupewa pesa nyingi na uongozi iwapo watapata matokeo mazuri hali iliyomfanya aamini angewafunga wapinzani wao.

 

“Tunashukuru mechi imeisha salama licha ya kufanikiwa kupata sare kwa sababu malengo yalikuwa ni kupata ushindi na ikizingatiwa uongozi umetupa ahadi ya kutupa zawadi ya pesa, siwezi kusema kiasi gani, kwa matokeo yoyote mazuri ambayo tutaweza kuyapata.

 

“Simba ni timu nzuri na ina wachezaji wazuri, maana kwangu ni mara ya kwanza kucheza nao, nimejisikia furaha kuwafunga kwa sababu niliamini nitafanya hivyo tangu wakati tupo hotelini ingawa hofu yetu ilikuwa upande wa Shiza Kichuya kutokana na ubora wake,” alisema Blaise.

Ibrahim Mussa, Dar es Salaam.

Comments are closed.