The House of Favourite Newspapers

Msolla: Tungewafunga, Lile ‘Bao la Mwamuzi’

0

MWENYEKITI wa Yanga, Dk Mshindo Msolla ameweka wazi walikuwa na nafasi kubwa ya kuwafunga wapinzani wao Simba lakini hilo lilishindikana kutokana na mwamuzi kuwapa bao lisilo la halali.

 

Msolla amesema hayo baada ya timu yake kutoka sare ya mabao 2-2 na Simba katika mechi ya Kariakoo Derby ambayo ilipigwa juzi Jumamosi katika Uwanja wa Taifa jijini Dar.

 

Katika mechi hiyo mabao ya Yanga yalifungwa na Balama Mapinduzi dakika ya 49 na Mohammed Issa ‘Banka’ dakika ya 52.Katika mechi hiyo, Simba walipata penalti dakika ya 38 baada ya Kelvin Yondani kumuangusha Meddie Kagere kisha Kagere kufunga penalti hiyo dakika ya 42. Bao lingine la Simba lilifungwa na Deo Kanda.

 

Dk Msolla ameliambia Championi Jumatatu, kuwa walikuwa na uwezo wa kushinda mechi hiyo baada ya kusawazisha mabao yote mawili kutokana na mpango waliokuwa nao lakini wenzao wamshukuru mwamuzi Jonesia Rukyaa ambaye aliwapa penalti ambayo haikuwa halali.

 

“Lile bao mwamuzi aliamua kuwapa, kwa sababu faulo ilifanyika nje, mchezaji akaangukia ndani ila bao la pili limefungwa halali.

“Lakini sisi tulikuwa na mpango ambao unaeleweka na tulicheza bila ya kujilinda ndiyo maana tukarudisha mabao yote mawili.

 

“Tulikuwa na motisha kubwa sana, mechi kama hii kutoka nyuma mabao mawili si rahisi na ninawapongeza wachezaji kwa kuwa walifuata maelekezo ya mwalimu, nawapongeza kwa kufanya kazi kubwa.

 

“Kama mwamuzi angekuwa ‘fair’ tungeshinda mechi hii kwani ile penalti haikuwa halali ila kwetu hii ilikuwa kama mechi nyingine za ligi, akili yetu sasa ni mechi nyingine zinazokuja na tunataka kufanya vizuri ili tusogee juu kuliko tulipo hapa sasa,” alisema Dk Msolla.

SAID ALLY, Dar es Salam

Leave A Reply