The House of Favourite Newspapers

Muivory Coast wa Yanga, Balaa Lake Watakoma!

0

STRAIKA mpya wa Yanga, Muivory Coast, Ykiep Gnaimen, unaambiwa ni hatari wa kupiga mashuti ya mbali kuanzia mita 18-20 na juzi mazoezini, aliwakomesha makipa wa timu hiyo, Farouk Shikalo, Metacha Mnata na Ramadhani Kabwili.

 

Muivory Coast huyo mwenye umbo kubwa, hivi karibuni alitua nchini kwa ajili ya kujiunga na timu hiyo katika usajili huu wa dirisha dogo lililofunguliwa Desemba 16, mwaka huu baada ya kuvunja mkataba wake Gor Mahia ya nchini Kenya.

 

Straika huyo hivi sasa yupo kambini akijifua huku akisubiria kusaini mkataba wa kuichezea timu hiyo ambayo tayari imesajili wachezaji wanne ambao ni Ditram nchimbi, Tariq Seif, Adeyum Salehe na Haruna Niyonzima.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatatu kutoka ndani ya benchi la ufundi la timu hiyo, achana na sifa yake ya kufunga mabao ya vichwa, nyingine ni ya kufunga kwa mashuti makali ya umbali wa mita 18-20.

 

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa katika kambi ya mkoani Mbeya ilipokwenda kucheza michezo yake miwili ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons, mazoezini aliwashtua makipa na makocha wa timu hiyo kutokana na umahiri wake wa kupiga mashuti makali.

 

Aliongeza kuwa wakiwa mazoezini, Kaimu Kocha Mkuu wa timu hiyo, Charles Mkwasa aliwapa program ya kupiga mashuti ya umbali wa mita 18-20 ambayo Muivory Coast huyo alionyesha umahiri wake hali iliyosababisha makipa hao kumkimbia kila inapofikia zamu yake ya kupiga.

 

“Shikalo ndiye alikuwa kipa wa kwanza kumkimbia mshambuliaji huyo kila inapofikia zamu yake katika kupiga, ni mshambuliaji mwenye uwezo mkubwa wa kupiga mashuti.

 

“Yanga ilikosa mshambuliaji mwenye uwezo kama wake wa kupiga mashuti ya umbali wa mita hizo 18-20, hivyo ujio wake ndani ya Yanga ni faida kubwa katika timu.

 

“Mshambuliaji huyo alionyesha umahiri wake wa kupiga mashuti wakati timu ilipokuwa kambini Mbeya, hiyo ni sifa yake ya pili aliyokuwa nayo tofauti na ile ya kupiga mipira ya vichwa,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Mkwasa alimzungumzia mshambuliaji huyo kwa kusema: “Ni mshambuliaji mzuri mwenye uwezo mkubwa wa kufunga mabao kwa kichwa na kupiga mashuti, lakini nahitaji muda zaidi wa kumuangalia.”

Leave A Reply