The House of Favourite Newspapers

Mwakalebela aahidi kuiendesha Yanga kisayansi

MGOMBEA nafasi ya Umakamu Mwenyekiti, Fredrick Mwakalebela ameahidi kuiongoza klabu hiyo kisayansi mara baada ya kufanikiwa kushinda katika nafasi hiyo.

 

Kauli hiyo, aliitoa juzi wakati wa uzinduzi wa kampeni zake zilizofanyika Makao Makuu ya Yanga mitaa ya Jangwani jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Mwakalebela alisema klabu hiyo hivi sasa inatakiwa kuendana na wakati kwa kuhakikisha inaendeleshwa kisayansi zaidi ya ilivyokuwa sasa.

 

Mwakalebela alisema katika kufanikisha hilo ni muhimu wanachama kuwaweka viongozi wenye uwezo na uzoefu wa kuiongoza klabu hiyo kwa lengo la kupata mafanikio zaidi.

 

Aliongeza kuwa, binafsi yeye ana uwezo na uzoefu huo alioupata tangu akiwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) akiongoza akiwa kama katibu na Leodegar Tenga akiwa ni rais.

 

“Nalifahamu vizuri soka la kitaifa na kimataifa kama unavyofahamu niliwahi kushika moja ya nafasi za juu zaidi katika uongozi wangu wa soka kitaifa nikiwa katibu mkuu wa TFF.

 

“Nikiwa katibu kulifanya soka la Tanzania kukubalika kwa Serikali na kwa wananchi, hivyo basi uwepo wangu Yanga utafanikisha baadhi ya vitu ikiwemo kuiongoza klabu kisayansi.

 

“Nafahamu siyo kazi rahisi, lakini kwa kupitia mwenyekiti wangu na wajumbe nitafanikiwa, pia nitasaidia kutafsiri baadhi ya kanuni na sheria za TFF, Caf na Fifa ambazo ninazifahamu nilizozifahamu nikiwa katibu wa TFF,” alisema Mwakalebela.

Comments are closed.