Mwalimu bora duniani kutoka Kenya akutana na Trump
BROTHER TABICHI ni mtawa wa Shirika la Kikatoliki la Mtakatifu Fransisco wa Capuchini na alishinda tuzo ya mwalimu bora duniani mnamo Machi 2019.
Mwalimu huyo anafundisha sayansi katika Shule ya Sekondari ya Keriko katika kaunti ya Nakuru, kaskazini-magharibi mwa mji mkuu wa Kenya, Nairobi.
Picha ya Tabichi akikutana na Rais wa Marekani, Donald Trump, iliyowekwa na ofisa wa mawasiliano kutoka Ikulu ya Marekani, kwenye Twitter, imesema Tabichi alitoa asilimia 80 ya mshahara wake kwa mwezi kuwasaida masikini nchini mwake, Kenya.
“Uwajibikaji wake na kazi yake ngumu na imani kwa wanafunzi, umeifanya shule anayofundisha kuibuka kidedea baada ya kushindana na shule zingine bora nchini katika mashindano ya kitaifa ya sayansi. Peter, unatutia moyo sisi sote! Asante kwa uwajibikaji wako kwa wanafunzi wako,” alisema Stephanie Grisham ofisa wa Ikulu ya Marekani.
Tabichi anatarajiwa kutoa maombi kabla ya kuanza kwa kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York baadaye leo. Anatarjiwa pia kuzungumzia kidogo kuhusu namna alivyofanikiwa kufika alipofika katika taaluma ya ualimu.
Tabichi amenukuliwa akisema kwamba: “Hii ni heshima kubwa kwa watawa wa St Franciscan. Inaonyesha kuwa Umoja wa Mataifa unatutambua kutokana na kwamba ina jukumu kuu katika kuendeleza utu.”
Comments are closed.