The House of Favourite Newspapers

Mzee Dalali: Emmanuel Okwi Bado Mashine Hatari

0
Mwenyekiti wa zamani wa Simba, Mzee Hassan Dalali.

MWENYEKITI wa zamani wa Simba, Mzee Hassan Dalali ameibuka na kufunguka kuwa kamati ya usajili ya timu hiyo haikukosea kumsajili tena mshambuliaji Mganda, Emmanuel Okwi kutokana na kuonyesha bado ni mashine hatari licha ya kubezwa na wapinzani wao Yanga kwa kumuita mhenga.

 

Okwi amejiunga na Simba kwa mkataba wa miaka miwili akitokea SC Villa ya Uganda, kabla ya hapo alikuwa akiitumikia Klabu ya Sonderjysk ya nchini Denmark.

 

Tayari mshambuliaji huyo ameshafikisha mabao sita katika mechi mbili za ligi alizocheza mpaka sasa ikiwa ni wastani wa mabao matatu kwa kila mechi huku akijinyakulia Tuzo ya Mchezaji Bora wa Agosti.

Mshambuliaji Mganda, Emmanuel Okwi.

Akizungumza na Championi Jumatano, Mzee Dalali alisema kwa upande wake bado anaona Okwi bado ni hatari kutokana na kufunga mabao sita hivyo hafanani na kuitwa mhenga kwa kuwa ubora wake umekuwa ukionekana.

 

“Simba ya msimu huu kiukweli ni nzuri, nawapongeza kamati ya usajili kwa kujaribu kuleta uwiano ambao mashabiki na wanachama wa Simba walikuwa wakiuhitaji siku nyingi na suala la Okwi kuitwa mhenga hilo haliwezi kutupa shida kwa sababu kitu cha msingi ni kwamba bado mashine.

 

“Unajua wakati nilipokuwa mwenyekiti ndiyo tulimsajili Okwi mwaka 2009 akiwa kijana mdogo sasa huo uzee wanaousema wapinzani wetu umeanza lini labda kwa kuwa amecheza ligi ya hapa kwa muda mrefu.

 

“Lakini bado ni mchezaji hatari kwa sababu hata wao ukiangalia safari hii timu yao haitishi kabisa ipo kama tunda la shokishoki yaani lina miba mingi lakini haichomi,” alisema Mzee Dalali.

Stori: Ibrahim Mussa | Championi Jumtano

Leave A Reply