NBC Kinara Taasisi za Fedha Maonyesho ya Nanenane
Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imekamilisha ushiriki wake kwenye Maonesho ya Kilimo Nanenane yaliyokuwa yakifanyika katika Uwanja wa John Mwakangale mkoani Mbeya kwa mafanikio makubwa ikiibuka kinara wa tuzo ya kundi la taasisi za fedha na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii zilizoshiriki maonesho hayo Kanda ya Kusini.
Katika Maonesho hayo yaliyohitimishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Samia Suluhu Hassani jana, ilishuhudiwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw. Theobald Sabi akikabidhiwa tuzo na waandaaji wa maonesho hayo ikiwa ni ishara ya kutambua umahiri, mchango na ushiriki wa taasisi hiyo katika kufanikisha maonesho hayo ya wadau wa kilimo.
“Tuzo hii ni uthibitisho kuwa jitihada kubwa zinazofanywa na Benki ya NBC kuhakikisha kwamba tunakuwa karibu zaidi na wadau wa kilimo kwa namna mbalimbali ikiwemo utoaji wa huduma zetu hadi ushiriki wetu kwenye shughuli zinazowahusisha wadau wa kilimo zinatambulika na kuthaminika vizuri mbele ya wadau…tunashukuru sana waandaaji wa maonesho haya kwa heshima waliyotupa nasi tunaahidi kundelea kuwa karibu nao pamoja na wadau wote wa kilimo kwa ujumla,’’ alisema Bw Sabi.
Akizungumzia ushiriki wa benki hiyo kwenye maonesho hayo Bw Sabi alisema ni muendelezo wa jitihada za benki hiyo katika kuendeleza na kukuza sekta ya kilimo hapa nchini kupitia mpango wake mahususi unaofajamika kama ‘NBC Shambani’ ukihusisha mnyororo wote wa sekta ya kilimo kuanzia kwa mkulima, mchakataji wa mazao ya kilimo hadi msambazaji kuendelea kujiweka karibu zaidi na wadau wa sekta hiyo muhimu.
“Kupitia Maonesho haya tumepata fursa ya kutangaza huduma zetu zinazohusiana na sekta nzima ya kilimo pamoja na kupokea mrejesho wa huduma hizo kutoka kwa wakulima na wadau wengine wengi wakiwemo viongozi mbalimbali waliotembelea banda letu wakiwemo wakuu wa mikoa na wilaya, wabunge, Mawaziri na viongozi wengine waandamizi wa kitaifa akiwemo Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano Dkt.Tulia Ackson.’’
“Wote hawa walitoa maoni yao na walionesha kuvutiwa na huduma zetu. Tunaahidi kuyafanyia kazi maoni yote waliyotupatia …tunawashukuru sana ’’ alisema Sabi.
Kwa upande wake Mkuu wa kitengo cha wateja wadogo wadogo, Lariba na wakulima kutoka Benki ya NBC Bw Raymond Urassa alisema tangu kuanza kwa maonesho hayo hadi kukamilika kwake wamefanikiwa kukutana na wadau mbalimbali wa sekta hiyo muhimu huku wengi wakionesha kuvutiwa zaidi na na huduma ya Bima ya Kilimo inayotolewa na benki hiyo pekee hapa nchini kwa kushirikiana na kampuni ya Bima ya Jubilee Insurance.
“Bima hii inalenga kuwalinda wakulima, wavuvi na wafugaji nchini dhidi ya hasara pindi wanapopata majanga mbalimbali yanayoweza kuathiri uzalishaji wao. Tunashukuru kuona kupitia maonesho haya wadau wameonesha kuipokea vizuri zaidi hali ambayo inazidi kutupa nguvu zaidi na ari ya kuendelea kubuni huduma mpya. Tunaamini kwamba kupitia maoni tuliyoyapata kutoka kwa wadau waliotutembelea siku chache hizi yatatuwezesha kubuni huduma bora zaidi zinazoendana na mahitaji ya wadau husika,’’ aliahidi.
Ushiriki wa Benki ya NBC kwenye maonesho hayo ulivutia wadau mbalimbali waliotembelea banda la benki hiyo akiwemo Dkt Tulia ambae alionyesha kuvutiwa zaidi na huduma ya Bima ya Kilimo.
“Pamoja na huduma zote nzuri mnazozitoa benki ya NBC kwa wakulima nimevutiwa sana na huduma ya Bima ya kilimo kwa wakulima. Nimevutiwa zaidi baada ya kusikia tayari kuna wakulima wa tumbaku huko mkoani Tabora wameshanufaika na huduma hii. Hiki ni kithibitisho tosha kuwa huduma hii inatekelezeka…hongereni sana kwa kuonesha njia,’’ alipongeza Dkt Tulia.
NA MWANDISHI WETU