The House of Favourite Newspapers

Ndoa ya Harmo, Sarah Yadaiwa Kuvunjika

0

NDOA ya msanii wa muziki wa Bongo Fleva, Rajabu Abdul ‘Harmonize’ au Harmo na mkewe Sarah Michelotti ipo gizani na kwamba wawili hao wameachana ndiyo habari ya mjini.

 

Ukijaribu kuwabishia wanaoeneza uvumi huo kwenye mitandao ya kijamii, watakuuliza “lini umewaona wakiwa pamoja!”

Ni ukweli usiopingika kwamba Harmo na Sarah siku hizi wameadimika kuonekana pamoja na habari zinadai kuwa mwanamke huyo ameshatimkia nchini kwake Italia.

 

Hata hivyo, Meneja wa msanii Harmo, Beauty Mmari alipoulizwa na mwandishi wetu kuhusu ndoa ya msanii wake kuvunjika alisema:“Kwanza watu wanatakiwa watambue kitu kimoja kwamba yale ni maisha yao binafsi, lakini kuhusu Harmonize kuachana na mke wake si kweli.

“Sema sisi kama uongozi tuliona tubadilishe mfumo wa maisha yake (lifestyle) aliyokuwa akiishi mwanzo.“Hivyo tukakaa kama uongozi na kuona siyo vizuri kila sehemu anayoenda Harmo, Sarah naye awe nyuma yake.

 

”Wakati Meneja wa Harmo akifafanua hayo, Sarah kwenye ukurasa wake wa Instagram hivi karibuni aliandika:“Kulipiza visasi sio jambo ninalolipendelea, utabaki na ujinga wako mwenyewe, habari za asubuhi.

 

”Waunganisha doti walipoona posti hiyo wakasema “hakuna mwingine anayeambiwa maneno haya ni Harmo.” Hata hivyo, Harmo hakujibu kitu na kuwaacha wananzengo wazidi kujiongeza wenyewe huku yeye akidili zaidi na uzinduzi wa wimbo wake mpya unaoitwa ‘Ushamba’ ambao umekuwa gumzo mtandaoni.

 

Mshamba wa Harmo aliyemtungia wimbo ni nani? Ni suala la kusubiri atakayelia kutoka gizani kwani wengi wamehusisha sehemu ya mashairi ya wimbo huo kuwa imelenga kumtupia madogo bosi wake wa zamani Nasibu Abdul ‘Diamond’.

 

Aidha, uchunguzi uliofanywa na Risasi umebaini kuwa mbali na Sarah kushindwa kufika kwenye uzinduzi wa wimbo wa Ushamba pia amefuta jina la Mrs Harmo alilokuwa akijiita awali katika akaunti yake ya Instagram.

 

Vipi kajipa talaka mwenyewe au kakinai kuitwa mke wa Harmo unabaki kuwa udadisi tu wa kichokozi ambao mwenye kujua ukweli wake ni mwanamke huyo raia wa Italia.

 

Harmo na Sarah wanadaiwa kufunga ndoa ya siri Septemba 7, mwaka jana jijini Dar es Salaam na kufanya sherehe iliyohudhuriwa na watu wachache jambo ambalo liliwafanya wengi kuingiwa na hisia hasi kuwa huenda wawili hao walikuwa wanatafuta kiki.

STORI: MEMORISE RICHARD, RISASI

Leave A Reply